Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 7 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 86 2018-09-12

Name

Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Primary Question

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-
Mgogoro wa ardhi kati ya Mbuga za Wanyama Selous – Kilwa na wananchi wanaoishi karibu na mbuga hiyo umezidi kuwa mkubwa kwa sababu mipaka halali haijulikani. Kwa mfano, mwaka 1974 mpaka halali ulikuwa Mto Matandu, mwaka 2010 mpaka huo ulisogezwa kufikia Bwawa la Kihurumila katika Kijiji cha Kikulyungu:-
a) Je, Serikali iko tayari kuhakiki eneo hilo ili kuondoa mgogoro mkubwa uliopo kati ya Wanakijiji wa Kihurumila na Mbuga?
b) Je, Serikali iko tayari kutatua mgogoro uliopo kati ya wananchi wa Kilwa na Mbuga.

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka wa Pori la Akiba Selous uliwekwa kwa kuzingatia Tangazo la Serikali Na. 275 kwa mujibu wa Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Na. 12 ya mwaka 1974. Tangu wakati huo hadi sasa mpaka huo haujafanyiwa marekebisho yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa mpaka kati ya Kijiji cha Kikulyungu na Pori la Akiba la Selous unatokana na kijiji hicho kutokukubaliana na uhakiki wa mpaka wa pori hilo uliofanyika mwaka 2010 kwenye eneo la Wilaya ya Liwale kwa kuwatumia wataalam kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kuwa, Wizara yangu ilitembelea Pori la Akiba la Selous – Kanda ya Kusini Liwale tarehe 3 na 4 Agosti, 2018 na kukutana na wananchi na viongozi wengine wa Serikali ikiwemo Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa mgogoro huo. Kupitia ziara hiyo, wananchi sasa wameridhia kazi ya uhakiki ifanyike upya na kuhakikisha kuwa watatoa ushirikiano kwa wataalam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu itashirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; wanakijiji; na Halmashauri ya Mji kuhakiki mpaka wa Pori la Akiba Selous katika eneo la Kijiji cha Kikulyungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kutatua migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya wananchi, wawekezaji na maeneo yaliyohifadhiwa, Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wote katika uhakiki wa mipaka na uwekaji wa alama kwenye mapori yote nchini na kuandaa na kusimamia mipango ya matumizi bora ya ardhi.