Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 42 2018-09-07

Name

Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-
Kwa sasa kumekuwa na wimbi kubwa la upimaji wa viwanja kwenye Manispaa mbalimbali nchini.
• Je, kwa nini wananchi wanalazimishwa kuuza maeneo hayo kwa Manispaa na kulipwa bei ndogo badala ya kufanya zoezi hilo kwa ubia?
• Kwa sababu maeneo hayo mengi ni mashamba, je, Serikali haioni kufanya hivyo kunasababisha Watanzania kukosa kazi maana asilimia 75 ni wakulima?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Mipango Miji Namba 8 ya mwaka 2007 inaelekeza kuwa eneo lolote likishatangazwa kuwa ni eneo la upangaji yaani planning area linapaswa kupangwa kwa kuzingatia Sheria ya Upangaji Mijini. Wananchi wanaokutwa kwenye maeneo hayo wanatakiwa kutambuliwa, kuelimishwa na kushirikishwa katika hatua zote za upangaji hadi umilikishaji. Pia Sera ya Ardhi ya mwaka 1995, Sheria ya Upimaji wa Ardhi Namba 4 na Namba 5 za mwaka 1999 na kanuni zake za mwaka 2001 na Sheria ya Mipango Miji Namba 8 ya mwaka 2007 pamoja na kanuni zake na miongozo yake, zinaelekeza Mamlaka za Upangaji kufanya upangaji na upimaji kwa kushirikisha wadau wote muhimu katika kupanga, kupima na kumilikisha ardhi. Aidha, Sheria ya Utwaaji Ardhi Namba 47 ya mwaka 1967 pamoja na mambo mengine inazingatia mamlaka za upangaji miji uhalali wa kutwaa ardhi iliyopangwa na inayohitaji kupangwa kutoka kwa wamiliki na kuwalipa fidia kwa kufuata miongozo ya ulipaji fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera na Sheria za Ardhi zinaelekeza umuhimu wa kutathmini ardhi na maendelezo ya wananchi waliokutwa nayo na kulipwa fidia sambamba na kupima na kumilikisha kwa makubaliano yatakayoridhiwa na pande zote mbili bila kuathiri sheria. Hata hivyo uzoefu unaonesha kuwa mamlaka za upangaji hupenda kutumia njia ya kulipa fidia ya Ardhi na maendelezo hali ambayo imeleta malalamiko mengi kutoka kwa wananchi. Serikali inazielekeza mamlaka zote za upangaji kutowalazimisha wananchi kutumia njia moja ya kulipa fidia na badala yake wananchi washirikishwe kuchagua njia wanayoona inafaa kati ya kuingia ubia au kulipwa fidia.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yote ambayo yametangazwa kuwa ni maeneo ya upangaji yaani planning area yanapaswa kuendelezwa kwa kuzingatia Sheria ya Upangaji Mijini. Ni kweli kuwa kuna maeneo yanayotwaliwa na kuingizwa kwenye mpango ya kuendelezwa kimji ambayo ni mashamba ya wananchi. Mamlaka za Upangaji kwa kuwashirikisha wananchi wenye maeneo hayo hupanga matumizi mbalimbali yakiwemo makazi, kilimo cha mjini, viwanda vidogo vidogo, masoko, biashara kubwa na ndogo, huduma mbalimbali za kijamii kwa kutegemea maendeleo ya kimji na matakwa ya sheria. Kwa hatua hii wananchi huwa na fursa ya kupata kazi za kuwaingizia kipato kwa kupata viwango vya matumizi watakayo pendelea.