Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 39 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 330 2018-05-29

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M.CHEGENI aliuliza:-
Kwa muda mrefu kumekuwepo na migogoro mingi kati ya Hifadhi za Taifa na wananchi ambao ni wakulima na wafugaji hali inayosababisha uvunjifu wa amani:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa tatizo hili linapata ufumbuzi endelevu hasa maeneo ya Lamadi, Makiloba, Kijereshi na Nyamikoma katika Wilaya ya Busega?
(b) Baadhi ya wanyama kama tembo wamekuwa wakifanya uharibifu wa mali na mazao ya wananchi wanaoishi maeneo hayo. Je, Serikali inatoa tamko gani la kuzuia tatizo hilo?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya Lamadi, Mwakiloba, Nyamikoma na Kigereshi yanapakana na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Pori la Akiba la Kijereshi, hivyo kuna muingiliano kati ya wanyama pori na binadamu jambo linalosababisha migogoro. Aidha, maeneo yaliyohifadhiwa yanakabiliwa na changomoto nyingi ikiwemo uvamizi unaotokana na shughuli za kibinadamu kama kilimo na mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kumaliza tatizo la migogoro ya mipaka, Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, wananchi na wadau wengine, inayo nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba migogoro kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi inatatuliwa. Kazi hii inahusisha kuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi katika vijiji vyote vinavyozunguka hifadhi, kutoa elimu ya uhifadhi kwa wananchi, kuimarisha miradi ya ujirani mwema na kupitia upya mipaka iliyopo katika maeneo yenye migogoro. Kazi ya kupitia mipaka na kuweka vigingi kwa sasa itaendelea kwa ushirikishwaji wa wadau wote muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na madhara yanayosababishwa na wanyamapori hususan tembo, Serikali imechukua hatua mbalimbali ili kunusuru maisha na mali za wananchi waishio kando ya Hifadhi ya Serengeti na Pori la Akiba la Kijereshi kama vile kuimarisha Timu ya Udhibiti wa Wanyamapori Hatari na Waharibifu ambao inajumuisha watumishi kutoka Kikosi dhidi ya Ujangili Bunda, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Pori la Akiba Kigereshi na Halmashauri ya Wilaya, pia kwa kutumia ndege zisizo kuwa na rubani kwa ajili ya kufukuza tembo. Lengo ni kuhakikisha kwamba tukio lolote la uvamizi wa tembo linashughulikiwa kwa haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inaendelea kusizitiza kuhusu umuhimu wa kuepuka kufanya shughuli za kibinadamu kwenye shoroba za wanyamapori na maeneo ya mipaka ya hifadhi ya vijiji. Aidha, Wizara imeandaa kanuni za kutenga na kuhifadhi shoroba na maeneo ya mtawanyiko ili kuruhusu mwingiliano wa kiikolojia kati ya wanyamapori utakaoimarisha utofauti wa vinasaba pamoja na kuboresha ustawi endelevu wa bioanuai.