Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 36 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 311 2018-05-24

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-
Kumekuwa na ajali nyingi zinazotokana na vitendo vya baadhi ya Askari Polisi maarufu kama PT kuwakamata waendesha bodaboda wakiwa kwenye mwendo huku wakiwa wamebeba abiria. Hali hiyo hupelekea waendesha bodaboda na abiria kupata ajali mara kwa mara:-
Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kuwa ajali za kizembe zinazosababishwa na baadhi ya Askari Polisi zinakomeshwa?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa tafiti mbalimbali zilizofanywa na Jeshi la Polisi, ajali za barabarani husababishwa na vyanzo vikuu vitatu ambavyo ni vyanzo vya kibinadamu ambavyo husababisha ajali kwa asilimia 76, vyanzo vya kiufundi ambavyo vinasababisha ajali kwa asilimia 16 na vyanzo vya kimazingira ambavyo vinasababisha ajali kwa asilimia 8. Ni katika vyanzo vya kibinadamu ndivyo tunakuta kuna uzembe ambao pia uko wa namna nyingi.
Mheshimiwa Spika, baadhi ya vijana wetu waendesha pikipiki bado wana uelewa mdogo kuhusu sharia za usalama barabarani na wengine pikipiki zao zina mapungufu mengi ambayo huwafanya kutokujiamini wanapoendesha. Kutokana na sababu hizi na nyinginezo, waendesha pikipiki hujihisi wana makosa wakati wote wawapo barabarani na hivyo huwa na hofu ya kukamatwa na Askari Polisi.
Mheshimiwa Spika, ni wajibu wa Askari Polisi kuhakikisha kuwa sheria zinafuatwa na si kuvunjwa. Waendesha pikipiki wanapaswa kutambua hilo na wao kutimiza wajibu wao wa kufuata sheria. Hali ya kutambua kuwa wana makosa ndiyo huwafanya kukimbia askari hata kama askari hana lengo la kuwakamata, hivyo husababisha ajali za kizembe bila sababu.
Mheshimiwa Spika, ili kuepukana na ajali za kizembe, Serikali kupitia Jeshi la Polisi itaendelea kutoa elimu kwa waendesha pikipiki ili kuwajengea uelewa wa sheria za usalama barabarani. Elimu hii itasaidia kuondokana na dhana potofu iliyojengeka miongoni mwa waendesha pikipiki na wapanda pikipiki kutokutii sheria ama kusababisha vyanzo vya ajali barabarani kwa kuwakimbia Askari Polisi kwa hofu ya kukamatwa, hata kama hawana makosa.
Mheshimiwa Spika, aidha, natumia fursa hii pia kulielekeza Jeshi la Polisi nchini kutumia muda wao vizuri katika kuwaelimisha waendesha pikipiki kufuata sheria za usalama barabarani kwa ajili ya usalama wao na watumiaji wengine wa barabara.