Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 10 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 82 2016-05-02

Name

Eng. Atashasta Justus Nditiye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muhambwe

Primary Question

MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi wa kuwadhibiti wakimbizi hasa maaskari ambao hutoroka kambini Nduta na kwenda kujumuika na wananchi, hivyo kuhatarisha usalama wa wananchi?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Atashasta Nditiye, Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama inavyofahamika, nchi yetu imekuwa ikipokea wakimbizi kwa miaka mingi na kuwahifadhi katika Kambi na Makazi. Kwa mujibu wa Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998 kifungu cha 16 na 17 kinaelekeza kuwa wakimbizi wote wanaishi katika maeneo maalum yaliyotengwa kwa ajili yao na hawaruhusiwi kutoka bila kibali maalum.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kudhibiti wakimbizi hasa maaskari kutoka nje ya kambi, Serikali imejiwekea mikakati ya makusudi ikiwemo kuwagundua wakimbizi/askari kwa kuwafanyia usaili wa awali na wale watakaobainika hupelekwa katika Kituo cha Utenganisho cha Mwisa kilichopo mkoani Kagera ambako huwekwa chini ya uangalizi kwa kipindi cha miezi mitatu hadi sita.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Serikali kujiridhisha na mienendo yao, hutakiwa kukana uaskari na kuomba hifadhi upya kwa masharti ya kutokujihusisha na harakati zozote za kisiasa na kijeshi zilizopo nchini. Hata hivyo Ofisi za Wakuu wa Kambi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi hukusanya taarifa za kiintelejensia na kufanya doria na misako mara kwa mara kambini na nje ya kambi ili kubaini wakimbizi watoro na wanapobainika hushtakiwa na kuadhibiwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakimbizi.