Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 35 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 305 2018-05-23

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Wananchi wa Kata ya Nkandasi wamejitahidi kujenga Shule ya Sekondari ya Kata ya Milundikwa hadi kufikia Kidato cha Sita, lakini Serikali kupitia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeamua shule hiyo kuhamishwa mara moja kuanzia tarehe 1 Januari, 2017 ili kuliachia Jeshi:-
(a) Je, Serikali inatoa mchango gani katika uhamishaji na ujenzi mpya wa shule hiyo?
(b) Je, Serikali iko tayari kufanya tathmini ya miundombinu yote ya shule na majengo yaliyojengwa na wananchi na thamani hiyo kuitoa katika fedha taslimu kwa ujenzi mpya wa shule?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbuge wa Nkasi Kusini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Milundikwa lilikuwa ni Kambi ya JKT iliyokuwa ikiendesha shughuli za malezi ya vijana na uzalishaji mali kabla ya Serikali kusitisha mpango wa kuchukua vijana mwaka 1994. Wakati JKT linasitisha shughuli zake katika Kambi hiyo liliacha majengo ya ofisi na nyumba za makazi, baadaye Halmashauri ya Wilaya ilianzisha shule ya Sekondari ya Milundikwa na kuongeza miundombinu michache katika shule hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua ya kuliongezea Jeshi la Kujenga Taifa uwezo wa kuchukua vijana wengi zaidi mwezi Novemba mwaka 2016 Serikali ilitoa maelekezo kwa JKT kufufua makambi yaliyokuwa yameachwa mwaka 1994 likiwemo la Milundikwa. Kufuatia maagizo hayo ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Nkasi na Halmashauri ya Wilaya hiyo waliratibu na kusimamia utaratibu wa kuhamisha Walimu na wanafunzi waliyokuwa katika shule Milundikwa kwenda katika shule jirani. Baadhi ya wanafunzi walihamishiwa katika shule ya Sekondari ya Kasu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia maendeleo ya wanafunzi waliokuwa wakisoma katika Shule ya Sekondari ya Milundikwa mnamo tarehe 9 Februari, 2017 Wizara ya Ulinzi na JKT kupitia Makao Makuu ya JKT ilitoa mabati idadi 2,014 ili kuhakikisha kuwa vyumba vya madarasa vilivyokuwa vinaendelea kujengwa vinakamilika na kuanza kutumika. Wizara yangu itakuwa tayari kuendelea kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya katika kutoa vifaa vya ujenzi kadri uwezo utakavyoruhusu.