Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 33 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 278 2018-05-21

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-
Mwaka 2015 Serikali ilianzisha Mamlaka ya Mji Mdogo wa Igunga kwa lengo la kusogeza karibu huduma kwa wananchi na kuleta maendeleo, lakini tangu wakati huo hadi leo hii, Mamlaka hiyo haijapatiwa fedha za kujiendesha na kutoa huduma kwa wananchi:-
(a) Je, ni lini Mamlaka hiyo itatengewa bajeti ili iweze kujiendesha na kufanya kazi zake kwa ufanisi?
(b) Je, ni lini Mamlaka hiyo itapatiwa fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya mji huo na kujenga barabara za lami kilometa nne zilizokuwa zimeahidiwa na Mheshimiwa Rais wakati wa Kampeni za Uchaguzi za mwaka 2015?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Mji Mdogo huanzishwa kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa, Sura ya 287, kifungu 13 - 21. Pamoja na vyanzo vya mapato vya Mamlaka ya Mji Mdogo kuainishwa katika Sheria ya Fedha za Mamlaka za Serikali za Mitaa, Sura ya 290, kifungu cha (8), Mamlaka hizo siyo Mamlaka kamili na hufanya kazi chini ya usimamizi wa Halmashauri za Wilaya husika. Hivyo, Mamlaka ya Mji Mdogo Igunga imekuwa ikiandaa mipango na bajeti zake kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Igunga na imekuwa ikipata mgao wa fedha kama zipatavyo Halmashauri nyingine nchini kutokana na upatikanaji wa fedha.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliahidi kujenga barabara zenye urefu wa kilometa 4 na katika mwaka wa fedha 2016/2017 barabara ya lami yenye urefu wa kilometa 0.67 ilikarabatiwa kwa gharama ya Sh.287,068,098. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali itajenga barabara yenye urefu wa kilometa 1.164 kwa kiwango cha lami katika Mji Mdogo wa Igunga, Sh.406,664,816 zimeshapelekwa na mkandarasi amefikia 5% ya utekelezaji wa mradi. Serikali itaendelea kujenga barabara za lami Wilayani Igunga kupitia TARURA kwa kadri fedha zinavyopatikana.