Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 32 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 269 2018-05-18

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Serikali imeanzisha Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC)
kwa lengo la kutatua matatizo ya walimu.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha Tume hiyo ili ifanye kazi kikamilifu kama ilivyokusudiwa?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) imeanzishwa kwa Sheria ya Utumishi wa Walimu Namba 25 ya mwaka 2015 na kuanza kutekeleza majukumu yake rasmi tarehe 1Julai, 2016 kupitia Ofisi za Tume zilizopo katika Wilaya 139 za kiutawala ambazo zinasimamiwa na Makatibu Wasaidizi wa Wilaya. Majukumu ya tume yameainishwa katika kifungu cha 5 cha Sheria hiyo ambayo ni pamoja na kusimamia mikataba ya ajira za walimu, kuwapandisha madaraja na kuchukua hatua za kinidhamu, ikiwemo kusikiliza rufaa kutoka ngazi za chini, kuwatambua na kutunza kumbukumbu za walimu wa shule za msingi na sekondari, kusimamia mafunzo ya walimu walio kazini, kufanya tafiti mbalimbali zinazohusu utumishi wa walimu na kutathmini hali ya utumishi wa walimu na kusimamia maadili ya utumishi wa walimu.
Mheshimiwa Spika, huu ni mwaka wa pili tu wa uhai wa Tume hiyo ambayo bado ni changa. Mikakati mahususi ya Serikali ili kuiimarisha zaidi Tume hiyo ni ifuatayo:-
• Kuendelea kuipatia fedha ili iweze kutimiza majukumu yake ipasavyo. Mfano katika mwaka wa fedha 2018/2019 Bunge limeiidhinishia Tume ya Utumishi wa Walimu shilingi 12,515,260,520 kati ya hizo shilingi 7,893,115,025 ni za mshahara na shilingi 4,622,145,495 ni za matumizi mengineyo, ili Tume ipate vitendea kazi kama magari, samani za ofisi na pia kugharamia vikao vya mashauri ya nidhamu na vifaa.
• Kuipatia ofisi na watumishi wa kudumu, mfano, hadi sasa inao Makatibu Wasaidizi wa Wilaya 138 ambao wameshajengewa uwezo na mwaka ujao 2018/2019 wataajiriwa watumishi 45 wapya na wengine 145 watahamishiwa kwenye Tume kama uhamisho wa kawaida. Uimarishaji wa Tume hiyo utaendelea kufanyika ndani ya wigo wa sheria iliyoanzisha Tume hiyo.