Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 2 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 19 2016-01-27

Name

Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIBU SAID HAJI aliuliza:- Mheshimiwa Spika, Sheria za FIFA zimekataza mambo yanayohusiana na mchezo wa soka kupelekwa Mahakamani:-
(a) Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya makosa yanayofanyika katika klabu za soka?
(b) Je, ni kwa kiasi gani sheria hizi za FIFA zinakinzana na Sheria za nchi yetu?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Sheria za FIFA zinakataza mambo yanayohusiana na soka kupelekwa Mahakamani. Hatua hiyo inalenga kuwezesha masuala yote yanayohusiana na soka kuendeshwa kwa kufuata na kuzingatia taratibu na miongozo iliyowekwa na mamlaka za mchezo huo katika ngazi mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, aidha, hatua hiyo imewezesha mchezo wa soka kuchezwa na kupata matokeo kwa wakati na hivyo kuepusha mazuio ya Mahakama ambayo yanaweza kusababisha usumbufu usio wa lazima kwa washiriki wengine.
Mheshimiwa Spika, utaratibu huo unazifanya mamlaka mbalimbali zinazosimamia mchezo huo kuwa na Katiba zinazowawezesha kupokea, kusikiliza na kutoa uamuzi dhidi ya malalamiko, rufaa na kero za wadau wa klabu au chama cha soka husika.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatoa wito kwa vyama, vilabu na mashirikisho ya mpira wa miguu kuzingatia na kufuata taratibu zilizowekwa kwa mujibu wa Katiba zao ili kupunguza migogoro inayoweza kujitokeza katika uendeshaji na uendelezaji wa soka nchini.
(b) Mheshimiwa Spika, maendeleo ya michezo hapa nchini yanaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Baraza la Michezo ya mwaka 1967, kama ilivyorekebishwa na Sheria Na. 6 ya mwaka 1971. Sheria hii ni kongwe na ina baadhi ya mambo ambayo yanakinzana na Sheria za FIFA. Serikali inafanya mapitio ya sheria hiyo ili iendane na wakati kwa lengo la kuboresha na kuendeleza michezo nchini.