Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 27 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 223 2018-05-11

Name

Anatropia Lwehikila Theonest

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-
Jimbo la Segerea ni kati ya majimbo yaliyosahaulika katika miundombinu ya barabara na kupelekea mitaa mingi kuwa na madimbwi sugu na mafuriko kila mvua inaponyesha. Kadhia hii imepelekea barabara za mitaa kupitika kwa taabu na kupelekea foleni kubwa katika barabara ya Segerea mpaka barabara ya Mandela kwa kuwa ndiyo barabara pekee inayotumiwa na wananchi.
Je, ni lini jimbo hili litatengewa bajeti kwa barabara zake za mitaa kwa kiwango cha lami, changarawe na ujenzi wa mifereji?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya barabara inayoendelea kutekelezwa kwa kiwango cha lami sambamba na mifereji katika Jimbo la Segerea ina thamani ya shilingi bilioni 4.6 ambapo Halmashauri ya Manispaa ya Ilala imetoa shilingi bilioni 2.6 na shilingi bilioni 2.0 zimetolewa na Mfuko wa Barabara. Miradi ya barabara inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na barabara za Mnyamani kilometa 2.3 kwa shilingi bilioni 2.5; Tabata Barakuda – Chang’ombe kilometa 0.5 kwa shilingi milioni 744 na Tabata – Kimanga – Mazda kilometa 0.8 kwa shilingi bilioni 1.4.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Jimbo la Segerea limetengewa shilingi milioni 880 ambapo kati ya fedha hizo shilingi milioni 380 zitatengeneza kwa kiwango cha changarawe barabara za Bonyokwa – Kisukuru- Majichumvi; Tabata – Mawenzi – Kisiwani; Chang’ombe – Majichumvi; Chang’ombe - Mbuyuni, Guest Nyekundu – Jumba la Dhahabu na shilingi milioni 500 zitatumika kufanya usanifu na ujenzi wa madaraja ya Mongolandege na Nyebulu.