Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 20 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 170 2018-05-02

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Serikali inakusudia kuyaondolea hadhi ya uhifadhi baadhi ya maeneo ya hifadhi kwa kuwa yamepoteza sifa hiyo. Kwa mujibu wa kauli ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akihutubia huko Benaco Wilayani Ngara, Mkoa wa Kagera mnamo tarehe 22 Desemba, 2015.
(a) Je, Serikali imeshaanza kuandaa mpango kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ili kuhakikisha kuwa kuna matumizi yenye tija na usawa baina ya wakulima na wafugaji pindi maeneo hayo yatakapokuwa huru ili kukuza uchumi na kuondoa hatari ya uvunjifu wa amani unaotokana na mgawanyo usio sawia kama ilivyo sasa?
(b) Je, kama Serikali imeshaanza kuandaa mpango huo, ipo tayari kuzishirikisha mapema Halmashauri za Wilaya zitakazoguswa na jambo hili ili nazo zianze kufanya maandalizi ya suala hili kwa ngazi yao?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya hifadhi yameanzishwa na kutangazwa kisheria kwa kuzingatia umuhimu wake kiikolojia, kiuchumi, kiusalama na kijamii kwa maslahi ya Taifa. Aidha, baadhi ya maeneo yanakabiliwa na uvamizi unaotokana na shughuli za kibinadamu kama kilimo na mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii imesababisha baadhi ya maeneo yaliyohifadhiwa kupoteza sifa ya kuendelea kuhifadhiwa. Kutokana na hali hiyo, Wizara yangu ilifanya tathmini ya maeneo hayo na kubaini jumla ya mapori tengefu 12 yalipoteza sifa na hivyo kuanzisha mchakato wa kuyarudisha kwa wananchi ili yatumike kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara yangu imepanga kufanya tathmini ya maeneo yaliyopoteza sifa kupitia Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI). Maeneo yaliyohifadhiwa pamoja na vitalu vya uwindaji wa kitalii yatafanyiwa tathmini ili kubainisha yale yote yaliyopoteza sifa za kuendelea kuwa hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya tathmini kukamilika, Serikali itaandaa mpango ambao utahusisha Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na Halmashauri za Wilaya ili kuhakikisha kuwa maeneo yatakayoondolewa hadhi ya uhifadhi yanatumika ipasavyo.