Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 20 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 168 2018-05-02

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Chuo cha Mahakama Lushoto (IJA) kinatoa taaluma ya Stashahada za Sheria.
(a) Je, ni lini sasa Serikali itaongeza uwezo wa Chuo hicho ili kitoe elimu ya sheria kwa ngazi ya Shahada?
(b) Je, ni kwa nini Serikali sasa isione umuhimu wa kukifanya Chuo hicho kiwe Wakala wa Law School ili mafunzo ya uwakili pia yaweze kutolewa chuoni hapo?

Name

Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, madhumuni ya kuwepo kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kutoa elimu endelevu kwa watumishi wa Mahakama na watumishi wa sekta nyingine za umma wakitokea kazini na siyo kutoa elimu ya sheria kwa ngazi ya shahada. Nia na makusudi hayo inalenga katika kuwaimarisha watumishi hao wanapokuwa kazini kwa kuwapatia mbinu na nyenzo muhimu ambazo ni nadra kupatikana wakati wanapokuwa shuleni/vyuoni na hivyo kuwasaidia katika kutekeleza majukumu yao ya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara bado tunaona kuwa kuna umuhimu wa kuendelea kusimamia lengo la kuanzishwa kwa chuo hicho kwani bado ni la msingi katika kuimarisha kitaaluma watumishi wa Mahakama na sekta nyingine nchini. Hata hivyo, kimeunda kikosi kazi cha kutafiti maeneo mapya ya uanzishwaji wa kozi mpya ikiwemo mafunzo ya ngazi ya Shahada ya Sheria katika Uongozi wa Mahakama (Bachelor of Law in Judicial Administration).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema, msingi wa kuanzishwa kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kutoa elimu kwa wanaotokea kazini ili kuwapatia nyenzo muhimu kuweza kutekeleza majukumu yao vema. Mafunzo yatolewayo na Chuo cha Uanasheria kwa vitendo yanalenga kumuandaa mhitimu wa shahada ya kwanza kutekeleza kazi ya Uwakili ya Uanasheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Chuo cha Lushoto lengo ni kumwongezea mbinu za kutekeleza kazi za kutoa haki yaani Mahakimu na Majaji, mafunzo ambayo yanatolewa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nachukua ushauri wa Mheshimiwa Mbunge ili kuangalia namna njema ya kuoanisha mafunzo yanayotolewa na vyuo hivi viwili.