Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 20 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 166 2018-05-02

Name

Daniel Nicodemus Nsanzugwako

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Primary Question

MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Katika nchi yetu suala la usawa na haki kwa wananchi wetu ni jambo linalozingatiwa sana na utawala wa Serikali ya Awamu ya Tano; taarifa ya hali ya umaskini nchini imebainisha kwamba ipo mikoa minne ambayo kiwango cha umaskini kipo juu sana na mojawapo ya mikoa hiyo ni Kigoma.
Je, ni hatua zipi za makusudi (kibajeti) zinazochukuliwa ili Mkoa wa Kigoma ujinasue na hali ya umaskini ambayo kwa kiasi cha asilimia 80 umesababishwa na madhila ya kihistoria (historical injustices) na Serikali kuacha au kushindwa kujenga miundombinu ya maendeleo kama barabara, vituo vya afya na kadhalika?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Wizara ya Fedha na Mipango, Idara ya Kuondoa Umaskini kwa kushirikiana na REPOA ilifanya uchambuzi wa kina wa hali ya umaskini kwa lengo la kupata takwimu za hali ya umaskini katika ngazi ya Mikoa na Wilaya (poverty mapping). Kwa mujibu wa takwimu zilizopatikana, Mkoa wa Kigoma ulikuwa na kiwango kikubwa cha watu wanaoishi chini ya mstari wa umaskini cha asilimia 48.9.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulitaarifu Bunge lako tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba siyo kweli kwamba Serikali iliacha au kushindwa kujenga miundombinu ya maendeleo kama barabara, vituo vya afya na kadhalika katika Mkoa wa Kigoma na hivyo kusababisha watu wa Kigoma kuwa maskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na Serikali katika Mkoa wa Kigoma ni pamoja na Daraja la Jakaya Kikwete katika Mto Malagarasi, Kivuko cha MV Malagarasi, barabara ya Kidahwe hadi Uvinza, Kigoma – Kidahwe na Mwandiga – Manyovu. Aidha, miradi ya barabara inayoendelea ni pamoja na Kidahwe – Kasulu, Kibondo – Nyakanazi na Kibondo – Mabamba mpaka mpakani mwa Burundi. Miradi mingine ni kukamilika kwa ujenzi wa majengo ya kitega uchumi ya NSSF na NHC, miradi ya umeme vijijini na uwanja wa ndege Kigoma awamu ya kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii yote imelenga kufungua fursa za kiuchumi kwa Mkoa wa Kigoma na hivyo kuongeza kasi ya kupunguza umasikini wa kipato kwa wananchi wa Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano (2016/2017 hadi 2020/2021), Serikali imepanga kuendeleza eneo maalum la uwekezaji Kigoma, upanuzi na uboreshaji wa bandari ya Kigoma, ujenzi na upanuzi wa uwanja wa ndege wa Kigoma, ujenzi wa mradi wa kuzalisha megawati 44.7 za umeme wa maji kutoka mto Malagarasi na kuunganishwa na Gridi ya Taifa ifikapo mwaka 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imepanga kujenga reli ya Kisasa na kuimarisha reli ya zamani na kununua vichwa 63 vya treni na mabehewa ya mizigo 1,960 kwa ajili ya kuimarisha shughuli za usafiri na usafirishaji kwa watu, bidhaa na huduma ifikapo mwaka 2020. Ni matarajio yetu kuwa kukamilika kwa miradi niliyoitaja kutafungua fursa za kiuchumi, kuongeza ajira na kupunguza umaskini kwa kiwango kikubwa katika Mkoa wa Kigoma.