Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 20 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 163 2018-05-02

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-
Ubora wa elimu wanayopata watoto wa jamii ya kifugaji wanaosoma shule za kutwa vijijini unaathiriwa sana na umbali mrefu wanaotembea wanafunzi kutoka makazi yao (maboma) hadi shuleni.
(a) Je, ni kwa nini Serikali isijenge mabweni katika baadhi ya shule zilizo kwenye vijiji vyenye mtawanyiko mkubwa wa maboma?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi wa Longido kujenga vyumba 177 vya madarasa, nyumba 291 za walimu na matundu 561 ya vyoo?
(c) Je, Serikali imepanga lini kuziba upungufu wa walimu 234; Waratibu Elimu Kata 18 na maafisa ngazi ya Wilaya 12 katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali refu la Mheshimiwa Dkt. Steven Lemomo Kiruswa, Mbunge wa Longido, lenye vipengele (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto inayowakabili watoto wa jamii ya kifugaji ndivyo maana katika kipindi cha kuanzia Julai, 2017 hadi Aprili, 2018 imekamilisha ujenzi wa bweni la wasichana na matundu 14 ya vyoo na inaendelea na ujenzi wa bweni la wavulana na nyumba tatu za Walimu katika Shule ya Msingi Sinya.
Vilevile nyumba ya Walimu two in one na madarasa matatu yanaendelea kujengwa katika Shule ya Msingi Kitumbeine ambao yatakamilika Juni, 2018.
Aidha, katika Shule ya Msingi Longido, ujenzi wa vyumba nne vya madarasa uko katika hatua ya msingi. Shule hizo tatu zina uwezo wa kuhudumia wanafunzi 1,323. Utekelezaji huo unafanyika ili kuwapunguzia adha watoto wa jamii ya kifugaji ambao kwa wastani hutembea zaidi ya kilometa 15 kutoka nyumbani hadi shuleni.
Aidha, ujenzi wa madarasa 24 kwenye Shule za Ranch, Imatiani Sokoni, Olmoti, Olmolog na Engurusai vimekamilika wakati ujenzi wa madarasa 18 katika shule mbalimbali unaendelea. Ujenzi wa bweni katika Shule ya Msingi Ngerenyai umekamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 515. Kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo, vyumba vya madarasa na nyumba za walimu. Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi na wadau itaendelea kujenga mabweni kwenye maeneo ya wafugaji na maeneo mengine yenye uhitaji kadri ya upatikanaji wa fedha utakavyowezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Longido ina Kata 18 ambazo kwa sasa Kata zote zina Maafisa Elimu Kata. Katika ngazi ya Halmashauri ya Wilaya kuna upungufu wa Afisa Elimu vielelezo baada ya aliyekuwepo kuhamishwa kwenda Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC). Serikali itaziba pengo hilo hivi karibuni, sambasamba na kupunguza upungufu wa walimu katika Shule za Msingi na Sekondari.