Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 16 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 130 2018-04-24

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Serikali imeunda timu ya wataalam kutoka Wizara nne kupitia nchi nzima kuangalia hadhi za hifadhi zetu (Mapori ya Akiba na Hifadhi za Msitu) ili kuja na mpango utakaondoa kabisa migogoro ya ardhi inayotokea kati ya Hifadhi na Wafugaji, Wakulima na Hifadhi na watumiaji wengine.
(i) Je, ni lini kazi hiyo itakamilika?
(ii) Je, mpaka sasa Timu hiyo imetembelea maeneo mangapi na ni mikoa gani?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali iliunda timu ya Kitaifa kwa ajili ya kushughulikia migogoro ya ardhi hapa nchini. Timu hiyo ilijumuisha wataalam kutoka Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Maliasili na Utalii, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Tume ya Taifa ya Takwimu.
Mheshimiwa Spika, kazi ya timu hii ni pamoja na kutembelea mikoa yote yenye migogoro; Kupitia na kuchambua kwa kina taarifa na mapendekezo yaliyowahi kutolewa na Kamati, Tume au timu mbalimbali kuhusu utatuzi wa migogoro nchini; Kuainisha vyanzo vya migogoro iliyopo; Kutembelea baadhi ya maeneo yenye migogoro ya muda mrefu pamoja na kukutana na wadau mbalimbali katika maeneo hayo; na Kutoa ushauri na mapendekezo ya utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi nchini.
Mheshimiwa Spika, mpaka sasa timu imefanikiwa kupitia taarifa mbalimbali za migogoro; kutembelea Wilaya 20, Halmashauri 24, Kata 40, Vijiji 74 na kufanya majadiliano na wadau 1,106 katika Mikoa ya Morogoro, Kagera, Geita, Tabora na Katavi. Taarifa ya Timu imekamilika na mapendekezo yamewasilishwa katika Wizara husika kwa utekelezaji.
Mheshimiwa Spika, jumla ya migogoro 1,750 ilifanyiwa uchambuzi. Kati ya hiyo 564 ilihusu uvamizi wa maeneo ya hifadhi; 218 mwingiliano wa mipaka ya kiutawala; 366 uanzishwaji wa vijiji ndani ya maeneo ya hifadhi; 204 migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji; migogoro 206 ilihusu wananchi na wawekezaji kwenye maeneo ya ranchi, mashamba na migodi; na migogoro 115 inatokana na madai ya fidia. Vilevile kulikuwa na migogoro 77 ambayo inatokana na mchanganyiko wa vyanzo mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara husika itaendelea kushirikiana na wadau wakiwemo wananchi kufanyia kazi mapendekezo ya timu ili kutatua migogoro ya matumizi ya ardhi iliyopo na inayoendelea kujitokeza nchini. Ni matumaini yangu kwamba utatuzi wa migogoro kwa njia shirikishi utasaidia kuondoa migogoro iliyopo kati ya wananchi, maeneo yaliyohifadhiwa na wawekezaji.