Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 16 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 129 2018-04-24

Name

Hawa Mchafu Chakoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani juu ya urithi wa Dunia wa Kisiwa cha Kilwa Kisiwani?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Kisiwa cha Kilwa Kisiwani kinapatikana katika Wilaya ya Kilwa Mkoa wa Lindi. Kisiwa hiki kina utajiri wa magofu ya kale yaliyoorodheshwa kwenye orodha ya Urithi wa Dunia mwaka 1981 na Shirika la Umoja wa Mataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni yaani UNESCO.
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha urithi wa Dunia wa Kilwa Kisiwani unaendelea kuwepo, Serikali imetekeleza mipango ifuatayo:-
(a) Kukarabati majenzi yaliyoorodheshwa kwenye Urithi wa Dunia. Ukarabati unafanywa na vijana wa Kitanzania kutoka Kisiwa cha Kilwa Kisiwani ambao wamepata mafunzo kutoka kwa wataalam wa UNESCO. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Wizara itajenga Ofisi itakayotumiwa na watumishi wa Urithi wa Dunia wa Kituo cha Magofu ya Kilwa Ksiwani na Songo Mnara.
(b) Kutangaza magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara ndani na nje ya nchi ili kuvutia watalii. Serikali imeandaa jarida la karibu Kilwa (Kilwa District heritage resources) linaloonyesha picha na maelezo ya vivutio vya utalii vilivyopo Wilayani Kilwa yakiwemo magofu ya Kilwa Kisiwani. Jarida hili linatolewa kwa wageni wanaotembelea Kilwa pamoja na kutumika kutangaza utalii wa Kilwa katika maonyesho ya ndani ya Sabasaba na Nanenane.
Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali sasa imeandaa mpango wa kuuza utalii wa malikale na wanyamapori kwa pamoja yaani one package. Kilwa Kisiwani itanufaika na mpango huu kwa kuunganishwa na package ya Pori la Akiba la Selou.
(c) Kushirikisha jamii ya Kilwa Kisiwani kuhifadhi na kujipatia kipato kupitia malikale zilizopo kwenye Urithi wa Dunia. Serikali itawapa fursa za ajira na mafunzo katika fani ya ukarabati wa majenzi, kuongoza wageni, huduma za chakula na fani nyingine za ujasiriamali. Elimu waliyoipata itawasaidia kuanzisha ofisi ya kuongoza wageni Kilwa Masoko na wengine wanafanya kazi za ukarabati wa magofu ya Urithi wa Dunia Kilwa Kisiwani.