Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 15 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 123 2018-04-23

Name

Zubeda Hassan Sakuru

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH L. HAULE (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-
Je, Serikali ina mikakati gani ya muda mrefu katika kuimarisha ushiriki wenye tija kwa Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kimataifa?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako naomba uniruhusu nitumie nafasi hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri kuipongeza timu yetu ya vijana ya Serengeti Boys kwa kuweza kufuzu kuingia mashindano ya nusu fainali katika mashindano ya CECAFA ambayo yanafanyika nchini Burundi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na timu zetu za michezo kuonesha kuwa matokeo yasiyoridhisha katika mashindano mbalimbali ya Kimataifa, dalili za Tanzania kurejesha sifa yake ya zamani ya umahiri katika michezo zimeanza kuonekana baada ya mwanariadha wetu nyota Alphonce Simbu kushika nafasi ya tano katika mashindano ya mbio ndefu za Olympic Brazil mwaka 2016. Simbu na wanariadha wengine wa Tanzania waliendeleza rekodi hiyo ya ushindi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Januari 2017, Simbu alinyakua medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Kimataifa ya mbio ndefu ya Mumbai – India; Aprili 2017 Cecilia Ginou Kapanga aliipatia Tanzania medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Beijing International Marathon nchini China; lakini vilevile tarehe 23 Aprili, 2017 Magdalena Chrispin Shauri alishika nafasi ya tano kati ya wanariadha 25,000 kwenye mashindano ya Hamburg Marathon nchini Ujerumani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Aprili, 2017 Emmanuel Ginouka Gisamoda alikuwa mshindi wa kwanza na kuipatia Tanzania medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Shanghai International Half Marathon. Lakini vilevile mwezi Aprili, 2017 Simbu alishika nafasi ya tatu kwenye mashindano makubwa ya London Marathon.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tumeona mafanikio yaliyojitokeza kwenye mchezo wa mpira wa miguu ambapo timu ya Taifa vijana Serengeti Boys ilifuzu kucheza fainali za michuano ya kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 nchini Gabon na kufuta historia hasi tuliyokuwa nayo ya timu zetu kushindwa kufika ngazi hiyo kwa miaka yote 37.
Mheshimiwa Mwenyekiti, somo kubwa tunalojifunza ni umuhimu wa mazoezi toka umri mdogo hivyo mkakati wa Serikali wa muda mrefu ni kama ifuatavyo:-
(i) Kuimarisha michezo shuleni ili kuibua na kulea vipaji vinavyojitokeza. Hivyo basi, shule 56 za sekondari zilizoteuliwa mwaka 2013 na mwaka 2014 na Serikali kila mkoa kuwa shule za michezo hazina budi kuimarishwa kwa vifaa, ufundishaji na miundombinu ili ziweze kutekeleza wajibu wake.
(ii) Katika kuimarisha uongozi katika vyama vya mashirikisho ya michezo mbalimbali nchini kwa kuvisimamia kwa karibu ili vizingatie katiba na sheria za michezo.
(iii) Kuimarisha mashindano ya UMITASHUMTA na UMISETA ambayo ndiyo kisima kikubwa cha kuwapata wanamichezo wa michezo yote nchini. Ahsante. (Makofi)