Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 11 | Sitting 15 | Health and Social Welfare | Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto | 122 | 2018-04-23 |
Name
Masoud Abdalla Salim
Sex
Male
Party
CUF
Constituent
Mtambile
Primary Question
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM aliuliza:-
Imebainika kuwa ugonjwa wa Kifua Kikuu (TB) umeendelea kuathiri jamii ya Watanzania.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kukabiliana na ongezeko la wagonjwa wa TB?
Name
Dr. Faustine Engelbert Ndugulile
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kigamboni
Answer
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim, Mbunge wa Mtambile, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, TB au Kifua Kikuu ni ugonjwa wa kuambukizwa na huambukizwa kwa njia ya hewa. Ugonjwa wa TB hushambulia mapafu na viungo vingine ikiwa ni pamoja na mifupa, uti wa mgongo, ubongo, moyo, ngozi na sehemu nyingine za mwili. Kwa ujumla TB inaweza kushambulia kila kiungo katika mwili. Ugonjwa huu husababishwa na vimelea aina ya bacteria na mgonjwa akitibiwa kwa dawa tulizonazo anaweza kupona kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu yeyote anaweza kuambukizwa au kuugua TB lakini makundi yafuatayo yako katika hatari kubwa zaidi kuugua ugonjwa huu ni pamoja na watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI, watoto wadogo chini ya miaka mitano, wazee, watu wanaougua magonjwa ya muda mrefu ikiwemo saratani, kisukari, wenye utapiamlo, wafungwa, wachimbaji wadogo wadogo migodini na wale wanaotumia madawa ya kulevya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumgundua mgonjwa wa TB mapema na kumweka katika matibabu ndiyo njia kuu ya kupambana na kushinda tatizo la kifua kikuu. Hivyo basi, mikakati ya Serikali imejikita katika afua za kuongeza uwezo wetu wa kuwafikia watu wote wanaohitaji huduma za TB ili kuwagundua wagonjwa hawa mapema na kuwatibu kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati na hatua zinazochukuliwa na Serikali ni kama ifuatavyo:-
(a) Kufanya upimaji wa TB kwa watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI;
(b) Kuingiza teknolojia mpya nchini ya upimaji na ugunduzi wa uhakika na uharaka wa vimelea vya TB kwa kutumia Gene Xpert. Hadi hivi sasa mashine 97 zimeshafungwa katika Hospitali za Mikoa na baadhi za Halmashauri na mashine nyingine 90 zimeshanunuliwa na zinatarajiwa kufungwa kwenye Hospitali za Wilaya zilizobakia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, teknolojia hii inawezesha sasa hivi badala ya siku za nyuma ambapo mgonjwa alihitaji kupima makohozi mara tatu kwa siku tatu, sasa hivi ugunduzi unaweza ukanyika ndani ya masaa mawili badala ya siku tatu kama ilivyokuwa awali.
(c) Tumewezesha maduka muhimu na Waganga wa Tiba Asili na Tiba Mbadala kufanya utambuzi wa dalili za TB na kutoa rufaa kwa wahisiwa wote kwenda katika mfumo wa tiba.
(d) Kufanya uchunguzi kwa wafanyakazi wote migodini na kwenye mahabusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena, Wizara yangu inatoa wito na kuwahimiza Waheshimiwa Wabunge kushiriki kikamilifu katika mapambano ya kutokomeza TB na kuhakikisha kwamba TB inakuwa ni ajenda yao ya kudumu katika vikao vyote vinavyoendelea na wanavyovihutubia.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved