Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 15 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 116 2018-04-23

Name

Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Primary Question

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza:-
Hospitali ya Wilaya ya Mbulu inakabiliwa na upungufu mkubwa wa watumishi; upungufu huo wa watumishi umeathiri utoaji wa huduma wa Hospitali hiyo na Vituo vya Afya vya Tawi na Daudi.
• Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza watumishi katika Hospitali hiyo?
• Serikali inatekeleza mpango wa upanuzi wa Vituo vya Afya zaidi ya 200 nchini; je, Serikali inachukua hatua gani kukabiliana na changamoto za watumishi, fedha na vitendea kazi?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya watumishi wa sekta ya afya katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu ni 345, watumishi waliopo ni 206 na upungufu ni watumishi 139. Serikali imeendelea kuajiri watumishi wa afya kadri wanavyohitimu na kupangwa moja kwa moja katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliajiri watumishi 2,058 wa kada za afya kwenye Mikoa na Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya hao, Halmashauri ya Mji wa Mbulu ilipangiwa watumishi kumi wakiwemo Madaktari wawili, Matatibu wawili; Afisa Muuguzi mmoja; Afisa Afya Mazingira mmoja na Msaidizi wa Afya, Mazingira mmoja; Mteknolojia Msaidizi mmoja na Wauguzi daraja la pili wawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri imeomba kibali cha kuwaajiri watumishi 91 ili kupunguza upungufu uliopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali inaendelea na ujenzi wa Vituo vya Afya 208 nchi nzima ili kuboresha huduma ya dharura kwa mama wajawazito. Ujenzi wa vituo hivyo utagharimu shilingi bilioni 132.9 hadi kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ujenzi huo, vituo hivyo vimetengewa shilingi bilioni 35.7 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na vifaatiba ili kuviwezesha kutoa huduma kwa wagonjwa. Katika mwaka wa fedha 2018/2019 Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeomba kibali cha kuwaajiri watumishi wa kada ya afya wapatao 25,000 ili kuhakikisha kunakuwepo na watumishi wenye sifa stahiki kwenye hospitali, vituo vyote vya afya na zahanati.