Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 11 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 94 2018-04-17

Name

Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI aliuliza:-
Wapo wananchi wengi waliotuhumiwa na kushtakiwa katika Mahakama tofauti na kutozwa faini na baada ya kulipa faini hizo wakakata rufaa Mahakama za juu kulalamikia hukumu hizo na Mahakama za juu zikawaona hawana hatia.
(a) Je, Serikali inayo kumbukumbu ya taarifa za wananchi wa namna hiyo?
(b) Na kama Serikali inazo taarifa hizo, je, ni lini wananchi hao watarejeshewa fedha zao?

Name

Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Roman Selasini, Mbunge wa Rombo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inazo kumbukumbu zote na taarifa za wananchi wanaolipa faini na baadae kushinda rufaa za kesi zao na hivyo kustahili kurejeshewa faini walizotoa kwani mashauri yote na hukumu zinazotolewa kumbukumbu zake zinatunzwa na Mahakama. Urejeshaji wa fedha hutegemea upatikanaji wa nyaraka zinazothibitisha malipo ya faini kupokeleawa na uwepo wa nakala ya hukumu kwani mara nyingi rufaa inaweza kuwa imetolewa baada ya muda mrefu tangu hukumu ya kwanza kutolewa.
Mheshimiwa Spika, utaratibu unaotumiwa na Mahakama ni kuwasilisha hazina nyaraka husika kwa ajili ya uhakiki na uidhinishwaji wa malipo kabla ya fedha zao kurejeshwa tena Mahakamani ili mwananchi husika aweze kulipwa. Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 na mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi 60,152,487.65 zililipwa na Mahakama kama fidia kwa mashauri 16 yaliyohakikiwa na kuthibitishwa na Mahakama baada ya kupokea fedha kutoka Hazina.
Mheshimiwa Spika, madai 24 yenye jumla ya shilingi 87,046,649.38 yameshachambuliwa na kuwasilishwa Hazina na tayari yanasubiri malipo na wakati huo huo jumla ya madai 12 yenye thamani ya shilingi 6,920,000 miongoni mwao yakiwemo madai mapya yamewasilishwa Hazina. Mara uhakiki utakapotengamaa na Mahakama kupokea fedha kutoka Hazina malipo hayo yatafanyika bila kuchelewa.
Mheshimiwa Spika, kama kuna mtu yeyote ambaye amecheleweshewa malipo yake nashauri awasiliane na Wizara au Mahakama ili kutatua tatizo hilo.