Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 78 2018-04-16

Name

Hamidu Hassan Bobali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mchinga

Primary Question

MHE. HAMIDU H. BOBALI aliuliza:-
Je, Serikali imefanya tathmini juu ya ubora na changamoto zilizopo katika shule za sekondari za kata nchini?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la kitafiti la Mheshimiwa Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka 1995 hadi 2005 ni kipindi ambacho tafiti, tathmini, mikakati na mipango mingi katika sekta ya elimu, ikiwemo Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu (ESDP) inayotekelezwa kupitia Mpango wa Elimu ya Msingi (MMEM) kuanzia mwaka 2000 na Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Sekondari (MMES) kuanzia mwaka 2004 ilianzishwa.
Mipango hiyo ndiyo chimbuko la maamuzi ya kuanzisha Shule ya Sekondari kila Kata ili kuhakikisha watoto wengi zaidi waliokuwa wanakosa nafasi za masomo ya sekondari, licha ya kufaulu mitihani ya darasa la saba kwa sababu tu ya uchache wa shule wanapata nafasi hizo. Hadi mwezi Oktoba, 2017 tulikuwa na shule za sekondari za kata 3,103 zilizokuwa na wanafunzi 197,663 ambapo kama zisingekuwepo wangeikosa elimu ya sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini mbili za Serikali zilizochambua kwa kina sekta ya elimu kupitia Tume ya Profesa Mchome ya mwaka 2013 iliyochambua sababu za ufaulu hafifu wa wanafunzi kwenye mitihani ya mwaka 2012 ya kidato cha nne na Kamati kuhuisha na kuoanisha Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 1995, Sera ya Elimu ya Ufundi na Mafunzo mwaka 1996, Sera ya Taifa ya Elimu ya Juu ya mwaka 1999 na Sera ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa Elimu ya Msingi mwaka 2007 iliyoongozwa na Mwalimu Abubakar Rajab mwaka 2013, ndizo zilizobaini na kuishauri Serikali kuanzisha sera mpya moja ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014.
Mheshimiwa Naibu Spika, sera mpya imetoa maelekezo mahususi kuhusu namna ya kuboresha elimu ya awali, elimu ya msingi, elimu ya sekondari, elimu ya ufundi na elimu ya juu. Mitaala imesharekebishwa, ikama, vifaa, samani na miundombinu vyote hivi vinaendelea kuboreshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa shule mpya, ujenzi wa madarasa, vyoo, maabara, mabweni, maktaba, nyumba za walimu, ofisi ya walimu, mabwalo na majengo ya utawala unaoendelea nchi nzima kwa kushirikiana na wananchi; kuboresha upatikanaji wa vitabu vya kiada na ziada katika shule za sekondari pamoja na juhudi za Serikali kuhakikisha walimu wa kutosha wanapatikana hasa wa masomo ya sayansi na hisabati, ni uthibitisho wa namna Serikali ilivyo na dhamira ya kuinua ubora wa elimu.