Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 77 2018-04-16

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:-
Kwa juhudi zake Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale ameanzisha ujenzi wa baadhi ya majengo ya zahanati kubwa na za kisasa katika Vijiji vya Nyamikonze na Inyenze.
(a) Je, Serikali ipo tayari kusaidia kukamilisha ujenzi huo?
(b) Je, Serikali ipo tayari kuifungua zahanati iliyojengwa na Mbunge katika Kijiji cha Mwamakilinga ambayo imekamilika tangu Novemba, 2014?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang’hwale, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Halmashauri ya Nyang’hwale kupitia mapato ya ndani ilitenga shilingi milioni 45 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati ya Kijiji cha Nyamikonze, lakini ukamilishaji haukufanyika kutokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Nyang’hwale kuwa kidogo. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Nyang’hwale kupitia mapato ya ndani imetenga shilingi milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Nyamikonze. Mpaka sasa zahanati haijaanza kufanya kazi na wananchi wa kijiji hicho wanapata huduma za afya katika zahanati ya Mwingiro iliyo karibu na kijiji hicho.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Nyang’hwale katika mwaka wa fedha 2017/2018 imetenga shilingi milioni 90 kutokana na mapato ya ndani kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati katika Kijiji cha Inyenze iliyofikia hatua ya kuezekwa. Fedha hizo bado hazijapatikana kutokana na makusanyo kuwa kidogo. Mara fedha hizo zitakapopatikana utekelezaji utafanyika kama mpango unavyoelekeza. Zahanati ya Mwamakilinga iliyojengwa na Mbunge wa Jimbo hilo, ilifunguliwa na Mheshimiwa Engineer Robert Gabriel, Mkuu wa Mkoa wa Geita tarehe 29 Januari, 2018 na mpaka sasa inafanya kazi.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale alianzisha ujenzi wa majengo matatu katika Kituo cha Afya Kharumwa ambayo yote yalikuwa hatua ya lenta. Majengo hayo ni wodi ya watoto, wadi ya wazazi ambayo ndani ina chumba cha upasuaji wa dharura kwa wajawazito na jengo la kuhifadhia maiti (mortuary). Shirika la AMREF linaendelea na ukamilishaji wa jengo la wodi ya wazazi ambayo ndani ina chumba cha upasuaji wa dharura kwa wajawazito. Ujenzi huo unategemea kukamilika ifikapo tarehe 15, Mei, 2018 kwa gharama ya shilingi milioni 164.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua jitihada kubwa zilizofanywa na Mbunge wa Nyang’hwale, mwishoni mwa mwezi Desemba, 2017 Serikali ilitoa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kukamilisha miundombinu ya Kituo cha Afya Kharumwa. Halmashauri imetenga shilingi milioni 70 kwa ajili ya ukamilishaji wa wodi ya watoto na shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa jengo la kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya Kharumwa. Ujenzi huo unaaendelea na unatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 30 Mei, 2018. Kiasi cha shilingi milioni 280 kilichobaki kitatumika katika ujenzi wa chumba cha upasuaji (theatre), maabara ya kisasa, nyumba ya mtumishi na wodi ya upasuaji (surgical ward) kwa wanawake na wanaume.