Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 7 Energy and Minerals Wizara ya Madini 59 2018-04-11

Name

Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Wananchi wa Msalala hususan wakazi wa Bulyanhulu wamefanyiwa dhuluma nyingi sana na Mgodi wa ACACIA, Bulyanhulu ikiwemo kuondolewa kwenye maeneo yao bila fidia mwaka 1996 na kwa wale wanaopata kazi mgodini kufukuzwa kazi bila kufuata utaratibu, kupata madhara makubwa ya kiafya na hata kusababishiwa vifo; na Serikali ya Awamu ya Tano imesimama kidete kutetea wananchi na kuwaepushia dhuluma hizi.
Je, ni hatua gani imefikiwa katika mazungumzo kati ya ACACIA na Serikali kuhusu ulipaji fidia kutokana na dhuluma hizo?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mgodi wa Bulyanhulu unamilikiwa na Kampuni ya ACACIA na unaendelea shughuli zake za uchimbaji madini tangu mwaka 2000. Kabla ya kuanzishwa kwa mgodi huo fidia stahiki kwa ardhi ya wananchi iliyotwaliwa ililipwa. Kwa sasa mgodi hauna madai yoyote ya wananchi wa Bulyanhulu yatokanayo na fidia ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2007 wafanyakazi wapatao 1,331 wa Mgodi wa Bulyanhulu walifanya mgomo kinyume cha sheria hivyo wakaachishwa kazi. Hata hivyo wafanyakazi 643 walirudishwa kazini. Tarehe 6 Novemba, 2007 wafanyakazi 658 waliogoma kurudi kazini walifungua kesi mahakamani na kuomba kufanyiwa uchunguzi wa kiafya ili kubaini hali za afya zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uchunguzi huo wafanyakazi 78 walionekana kuwa na matatizo ya kiafya. Kwa sasa kampuni ya ACACIA inajadiliana na Serikali kupitia OSHA na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kuhusiana na madai yao ya matibabu na fidia kulingana na sheria za nchi. Ili kupunguza magonjwa yanayohusiana na kazi za migodini Wizara inaendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu ili kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa kuzingatia usalama, afya mahali pa kazi, pamoja na utunzaji wa mazingira.