Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 6 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 49 2018-04-10

Name

Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Primary Question

MHE. PROSPER J. MBENA aliuliza:-
Kutokana na kuongezeka kwa matangazo ya biashara kwenye vyombo vya habari, upo uwezekano wa baadhi ya matangazo hayo kuwakera na kuleta hisia tofauti kwa baadhi ya watu na hasa watoto kutokana na maudhui mabaya ya baadhi ya matangazo haya.
(a) Je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kuunda chombo cha kusimamia maudhui ya matangazo ya kibiashara ili kuweka na kusimamia taratibu na kanuni za matangazo?
(b) Je, ni idara gani ya Serikali inahusika moja kwa moja na malalamiko ya wananchi dhidi ya kampuni na taasisi zinazotoa matangazo yenye athari kwa jamii?
(c) Je, ni hatua gani zinachukuliwa dhidi ya kampuni hizo?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prosper Joseph Mbena, Mbunge wa Morogoro Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tayari ina vyombo vya kusimamia maudhui ya vyombo vya habari nchini, yakiwemo maudhui katika matangazo. Vyombo hivyo ni Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inayoundwa chini ya kifungu cha Sheria Na. 4 cha Mamlaka ya Mawasiliano Na. 12 ya mwaka 2003, ambayo ina Kamati ya Maudhui iliyoundwa chini ya kifungu cha 26 cha sheria hiyo na marekebisho yake katika kifungu cha 173 cha Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroni na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010. Kamati hii ndiyo inayosimamia maudhui ya matangazo ya kielektroniki (redio, television na mitandao ya kijamii).
Mheshimiwa Naibu Spika, chombo cha pili ni Bodi ya Filamu Tanzania ambayo vilevile inasimamia maudhui katika picha jongevu zinazorushwa katika majumba ya sinema, hadharani vilevile katika michezo ya kuigiza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Habari Maelezo ni chombo cha tatu ambacho kimehuishwa chini ya kifungu cha Sheria Na. 4 na Sheria Na. 5 vya Sheria ya Huduma ya Habari Namba 12 ya mwaka 2016 kinachosimamia maudhui katika machapisho mbalimbali yakiwemo magazeti, majarida pamoja na vipeperushi.
Mheshimiwa Naibu Spika, zipo hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali inapobainika bila kutia shaka kuwa kampuni, asasi au taasisi imechapisha ama kutoa tangazo lenye athari kwa jamii. Hatua hizo ni pamoja na kupewa onyo, kufungiwa kutoa huduma kwa kipindi kitakachotajwa au kufungiwa kabisa kutokujihusisha na utangazaji au uchapishaji wa habari pamoja na matangazo. Serikali inaendelea kuhimiza jamii nzima kuendelea kuzingatia sheria na taratibu zilizopo katika kusambaza habari mbalimbali kwa jamii.