Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 45 2018-04-10

Name

Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Kuna uhaba wa nyumba za kuishi walimu licha ya juhudi za wananchi kujenga nyumba za walimu wa shule za msingi na sekondari; walimu hao pia wanahitaji kujenga nyumba zao wenyewe za kudumu.
Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu wa kutoa mikopo kwa walimu ili wajenge nyumba zao binafsi?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa upo uhaba wa nyumba za walimu katika shule za msingi na sekondari ndiyo maana imekuwa ikijitahidi kila mwaka kujenga nyumba za walimu. Katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 Serikali kwa kushirikiana na wananchi, imekamilisha ujenzi wa nyumba 274 za walimu na hivyo kufikisha idadi ya nyumba 14,640 kati ya nyumba 67,711 zinazohitajika kwenye shule za sekondari. Aidha, nyumba 290 za walimu zimejengwa kwenye shule za msingi na hivyo kufikisha idadi ya nyumba 45,638 kati ya nyumba 175,930 zinazohitajika. Takwimu hizo zinabainisha kwamba familia za walimu 52,071 katika shule za sekondari na familia za walimu 130,300 kwenye shule za msingi zinaishi kwenye nyumba za kupanga au nyumba zao binafsi. Ni wazi kwamba mahitaji ya nyumba za walimu ni makubwa mno.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kuendelea kuweka kipaumbele cha kujenga nyumba za walimu za kuishi familia mbili, nne au sita ambazo ni za gharama nafuu kulinganisha na gharama za kujenga nyumba za kuishi familia moja. Kipaumbele cha juu kitaendelea kuwekwa kwenye maeneo yenye mazingira magumu ya kupata nyumba za kupanga hasa maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa mikopo kwa ajili ya Walimu kujenga nyumba zao binafsi ni kama ulivyo kwa watumishi wengine wa Serikali, ambapo mtumishi anaruhusiwa kukopa kwenye taasisi au benki yenye mkataba maalum na mwajiri kwa kujaza fomu ili akatwe marejesho ya mkopo kutoka kwenye mshahara ambapo makato ya mkopo hayatakiwi kuzidi theluthi mbili ya mshahara na mkopo wote kulipwa kwa kipindi cha kati ya miezi 36 (miaka mitatu) hadi miezi 300 (miaka 25) kulingana na masharti ya taasisi husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa taasisi zinazotoa mikopo ya nyumba kwa watumishi wa Serikali wakiwemo walimu ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Kampuni ya Nyumba za Watumishi (Watumishi Housing Company), Benki ya Afrika (Bank of Africa – BOA) kupitia mpango wake wa WEZESHA, mabenki kadhaa mengine kama NMB, CRDB, Azania na kadhalika na kampuni nyingine kama vile T-Mortgage yanayolenga zaidi kuwakopesha watumishi wa kipato cha chini na cha kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili watumishi wakiwemo walimu wapate mikopo ya kujenga nyumba binafsi kwenye maeneo watakayochagua wao, inatakiwa Wakurugenzi wa Halmashauri wawasiliane na taasisi zinazokopesha ili waingie makubaliano maalum yatakayowawezesha watumishi wa Halmashauri wanaotaka mikopo ya kujenga nyumba binafsi wakiwemo walimu kupata mkopo.