Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 57 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 477 2017-06-30

Name

Mwantakaje Haji Juma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Bububu

Primary Question

MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA aliuliza:-
(a) Je, ni lini Serikali itawapatia gari lingine Kituo cha Polisi Magharibi ‘A’ ili kupunguza matumizi ya magari binafsi kwa Jeshi la Polisi?
(b) Je, Serikali imejipanga vipi kupunguza uhalifu unaojitokeza mara kwa mara?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Bububu lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la upungufu wa vitendea kazi katika Jeshi la Polisi hususan magari ya doria kote nchini ikiwemo Bububu. Kwa kuzingatia umuhimu wa doria katika kudhibiti masuala ya usalama wa raia, Serikali inaendelea kuongeza idadi ya magari na vitendea kazi vinginevyo kadiri hali ya uchumi inavyoruhusu. Mpango ya Jeshi la Polisi ni kupeleka gari moja katika Wilaya ya Magharibi ‘A’ mara baada ya kupokea magari mapya katika siku za hivi karibuni.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeendelea kutekeleza jukumu lake la msingi la ulinzi wa raia pamoja na mali zao ili kuhakikisha wananchi na mali zao wanakuwa katika hali ya usalama. Katika kutekeleza jukumu hilo ipo mikakati mbalimbali ambayo imetekelezwa ikiwa ni pamoja na kufanya doria na operesheni za mara kwa mara, kutoa elimu kwa jamii ili kuwajengea uwezo wa kutambua matendo yanayoashiria uhalifu na kutoa taarifa polisi kwa lengo la kuchukua hatua kabla uharibifu kufanyika. (Makofi)