Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 55 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 457 2017-06-28

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENAN aliuliza:-
Mara kwa mara Serikali imekuwa ikishindwa kesi mbalimbali Mahakamani:-
Je, Serikali imefanya uchunguzi na kujua sababu za kushindwa kesi mara kwa mara?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA NA VIJANA (K.n. y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenan, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge hakutaja aina ya kesi anazomaanisha katika swali lake, nianze kwa kufafanua kwamba, kuna aina mbalimbali za kesi au mashauri yanayofunguliwa Mahakamani na Serikali au dhidi ya Serikali. Mfano, mashauri ya jinai, madai, katiba, uchaguzi na kadhalika. Kwa ujumla mashauri hayo hufunguliwa kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, vilevile Halmashauri, Mashirika ya Umma, Taasisi, Wakala wa Serikali na Idara za Serikali zinazojitegemea zinayo mamlaka ya kuendesha na kusimamia mashauri yanayofunguliwa dhidi yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, mashauri yote yanayofunguliwa na Serikali au dhidi ya Serikali yamekuwa yakiendeshwa kwa weledi na pale inapostahili Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imekuwa ikiratibu uendeshaji wa mashauri hayo na takwimu zetu zinaonesha mashauri mengi Serikali inashinda. Kwa mfano, kati ya mashauri 53 ya kupinga Uchaguzi wa Ubunge yaliyofunguliwa Mahakamani baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, Serikali ilishinda mashauri 52 na kushindwa shauri moja tu na katika mashauri 199 ya kupinga Uchaguzi wa Madiwani, Serikali ilishinda kesi 195.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama takwimu zinavyoonesha si kweli kwamba, Serikali imekuwa ikishindwa kesi mara kwa mara. Hata hivyo, katika nchi yoyote inayozingatia uhuru wa Mahakama na utawala wa sheria, Serikali haiwezi kushinda kila shauri hata kama haistahili. Ni kweli kuna baadhi ya kesi ambazo Serikali inashindwa, sababu zinazosababisha Serikali kushindwa baadhi ya mashauri ni pamoja na namna ushahidi ulivyokusanywa na vyombo vya Serikali, kutokupatikana mashahidi muhimu, mashahidi kutokutoa ushahidi uliotegemewa, baadhi ya Taasisi, Mashirika ya Umma na Idara za Serikali kutoishirikisha mapema ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, zinapofungua au kufunguliwa mashauri Mahakamani, namna ushahidi unavyochukuliwa Mahakamani, mashahidi kula njama na kutoa ushahidi unaoathiri mashauri ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto hizo, Serikali imekuwa ikichukua hatua kadhaa ikiwemo kuhakikisha kuwa, mashahidi muhimu wanapatikana, kuwaandaa ipasavyo mashahidi kabla ya kutoa ushahidi, kujiandaa vema katika kila shauri, kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi ipasavyo, kushirikiana na vyombo vya Upelelezi kama TAKUKURU na Jeshi la Polisi katika maeneo yanayosababisha ushahidi kuwa hafifu na kurekebisha kasoro hizo, kukata rufaa na kuendelea kuzishauri taasisi za Serikali kutoa taarifa mapema kwa Mwanasheri Mkuu wa Serikali katika kila shauri lililofunguliwa Mahakamani, ili kwa pamoja kuangalia namna ya kulinda maslahi ya Serikali katika shauri husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kupitia Bunge hili sheria zinazosimamia Mashirika na Taasisi za Serikali zimekuwa zikirekebishwa na kuweka masharti yanayompatia Mwanasheria Mkuu wa Serikali haki ya kuingilia kati shauri lolote lililofunguliwa dhidi ya Serikali au Taasisi ya Umma kwa lengo la kulinda maslahi ya Serikali.