Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 46 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 375 2017-06-13

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Serikali yoyote duniani inaendeshwa na rasilimali watu wenye weledi, ari na uzalendo. Ili Watumishi hawa wafanye kazi kwa moyo wanahitaji kuthaminiwa, kutambuliwa mchango wao na kupewa stahili zao bila bughudha:-
Je, Serikali imebuni mkakati gani wa kuwapa motisha na ari Watumishi wa Umma ili wafanye kazi kwa kujituma badala ya vitisho?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, napenda kutoa maelezo kwamba utekelezaji wa shughuli za Serikali huendeshwa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo mbalimbali inayosimamia Utumishi wa Umma ambapo kila mtumishi hupaswa kuzingatia wakati wa kutekeleza majukumu yake. Hivyo, Serikali haitumii vitisho wala bughudha katika kusimamia watumishi wake, bali husimamia sheria, kanuni na taratibu hizo.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa Watumishi wa Umma ni rasilimali ya msingi katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu na malengo yake kwani nguvu na mafanikio ya Taifa lolote inategemea aina ya Watumishi lililonao na ni kwa msingi huo, Watumishi hawana budi kuendelezwa na kupewa motisha ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Kwa kutambua umuhimu wa motisha kwa Watumishi wa Umma, Serikali inayo mikakati mbalimbali inayolenga kuongeza ari kwa Watumishi wa Umma na hivyo kuwawezesha kufanya kazi kwa weledi na kwa kujituma. Mikakati hii ni pamoja na:-
(a) Kupunguza kiwango cha kodi ya mapato kwenye mshahara au Pay As You Earn kutoka asilimia 14 mwaka 2010/2011 hadi asilimia tisa mwaka 2016/17. Hatua hii imesaidia kuongezeka kwa kiwango cha mshahara anachobakinacho mtumishi baada ya kukatwa kodi.
(b) Kuongeza kima cha chini cha mshahara kutoka Sh.100,000/= mwaka 2010/2011 hadi Sh.300,000/= mwaka 2015/2016 sawa na ongezeko la asilimia 200.
(c) Kupitia Waraka Na. 3 wa mwaka 2011 unaohusu utaratibu wa kuwakopesha watumishi vyombo vya usafiri, Serikali imekuwa ikiwakopesha Watumishi vyombo vya usafiri ili kuwapunguzia adha ya usafiri wakati wa kwenda kazini na kurudi majumbani.
(d) Kutoa dhamana kwa watumishi wakati wanapokopa fedha katika Benki na Taasisi mbalimbali za kifedha.
(e) Kuanzisha Watumishi Housing Company Limited kwa ajili ya kujenga nyumba za gharama nafuu na kuwauzia au kuwakopesha Watumishi ili waishi kwenye makazi yenye staha.
(f) Kupitia sera ya mafunzo katika Utumishi wa Umma ya mwaka 2013, Serikali imekuwa ikitumia rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia mafunzo ya Watumishi wa Umma ili wawe na weledi wa kutosha.
(g) Serikali imekuwa ikiratibu nafasi za mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa Watumishi wa Umma kutoka kwa nchi na wadau wa maendeleo kama vile Ubelgiji, Uholanzi, Australia, Jamhuri ya Korea, Ujerumani, China, Japan, India, Malaysia, Indonesia, Singapore, Sweden na Jumuiya ya Madola na nchi zinginezo.
(h) Pamoja na Serikali kufanya zoezi la tathmini ya kazi kwa lengo la kubaini uzito wa majukumu ya Kada mbalimbali za Watumishi na hivyo kuwa msingi wa kupanga ngazi za mishahara. Zoezi hili linatarajiwa kukamilika katika mwaka 2017/2018.