Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 8 Public Service Management Ofisi ya Rais TAMISEMI. 64 2016-04-29

Name

Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Primary Question

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:-
Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa wana majukumu mengi ikiwemo kuhakikisha amani na usalama katika maeneo yao:-
Je, ni lini Serikali itaanza kuwalipa posho ya mwezi ya Wenyeviti hawa ili kutoa motisha kwa kazi yao?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kazi kubwa inayofanywa na Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa katika kusimamia shughuli za Maendeleo Nchini. Katika kuzingatia uzito huo wa majukumu, Serikali imeweka utaratibu wa kila Halmashauri kurejesha katika Vijiji na Mitaa asilimia 20 ya mapato ya ndani ambapo sehemu ya fedha hizo zinatakiwa kulipa posho ya Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kuwa baadhi ya Halmashauri hazipeleki fedha hizo katika Vijiji na Mitaa na hivyo kuwanyima haki Viongozi hao kulipwa posho zao. Changamoto kubwa ya Halmashauri ilikuwa ni makusanyo yasiyoridhisha ya mapato ya ndani ambayo yalisababisha kushindwa kulipa posho hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia sasa Serikali inaimarisha makusanyo ya mapato ya ndani kwa kutumia mifumo ya kielektroniki ambapo imethibitika kuongeza makusanyo kwa zaidi ya asilimia mia moja. Kwa njia hiyo, Halmashauri zitakuwa na uwezo wa kulipa posho za Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa ambao sote tunatambua mchango wao mkubwa katika Taifa hili wa kuhamasisha shuguli za maendeleo. Ofisi ya Rais, TAMISEMI, itaendelea kusimamia suala la makusanyo ya mapato ya ndani kwa nguvu zake zote ili kujenga uwezo wa Halmashauri kutekeleza majukumu yao kikamilifu.