Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 39 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 321 2017-06-01

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-
Mchango wa kazi za wasanii umeonekana katika kutoa ajira lakini bado wasanii wanakabiliwa na changamoto mbalimbali za kuhujumiwa kazi zao ambapo Mheshimiwa Rais ametoa maagizo mbalimbali ya kushughulikia watu wanaohujumu kazi za wasanii.
Je, mpaka sasa ni hatua gani zimechukuliwa?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Devotha naomba kwa ruhusa yako nichukue nafasi hii kutoa taarifa fupi ya mafanikio ya mrembo Aisha Mabula ambaye tulimuona hapa hivi karibuni Bungeni, aliewezeshwa na Waheshimiwa Wabunge kushiriki mashindano ya ulimbwende ya Miss World Super Model nchini China.
Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya washiriki walikuwa 52 kutoka nchi mbalimbali duniani lakini kutoka Afrika ni wawili ambapo mmoja wao ni huyo Bi. Aisha Mabula na Aisha Mabula alifanikiwa kuingia 14 bora kama fainali na katika fainali hiyo alishika nafasi ya tisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Bi. Aisha kwa kuiwakilisha vizuri nchi yetu ya Tanzania pamoja na Bara la Afrika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee kabisa niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa moyo wenu wa ukarimu ambapo mlimchangia na kumuwezesha kushiriki katika mashindano hayo ya kidunia ambayo naamini kabisa mafanikio haya yatamuwezesha kupata ajira na kuendelea kuitangaza nchi yetu Kimataifa na hasa katika sekta ya utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huu mfupi naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Kamati ya Urasimishaji wa Kazi za Filamu na Muziki nchini inayojumuisha Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Bodi ya Filamu Tanzania (TFB) na Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA) hutoa miongozo mbalimbali kuhusiana na masuala ya ulinzi na kazi za sanaa.
Aidha, kwa kushirikiana na COSOTA Wizara kupitia BASATA na Bodi ya Filamu Tanzania (TFB) hutoa copyright clearance certificate kwa mmiliki wa kazi yoyote ya sanaa kabla ya kupewa stempu ya kodi ya TRA. Lengo la stempu hizo ni kurasimisha sekta ya filamu na muziki katika uuzaji wa CD, DVD, kanda na kadhalika na hivyo kukabiliana na hujuma katika kazi za wasanii.
Mheshimiwa Naibu Spika, pale ambapo sheria na taratibu za forodha na za kulinda hakimiliki zinakiukwa na hivyo kuathiri maslahi ya wasanii, Serikali huendesha operesheni za kukamata kazi hizo za sanaa zenye utata. Hadi kufikia Machi 2017, Wizara ilifanya operesheni kubwa mbili na za kawaida sita dhidi ya filamu zinazoingia sokoni bila kufuata utaratibu ambapo jumla ya kazi 2,394,059 zilikamatwa zikiwemo kazi za nje ya nchi 2,393,529 zenye thamani ya zaidi ya shilingi 3,590,293,500 na za ndani 530 zenye thamani ya shilingi 1,590,000.
Aidha, mitambo ya kufyatua kazi za filamu (duplicators) 19, printers za CD/DVD nane, DVD writers 31, kompyuta tatu na UPS saba zilikamatwa katika operesheni hizo.