Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 2 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 17 2018-04-04

Name

Halima James Mdee

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA (K.n.y. MHE. HALIMA J. MDEE) aliuliza:-
Kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu sana unaohusu eneo lenye ukubwa wa ekari 357.5 Boko Dovya – Kawe – Kinondoni baina ya wananchi na watu wanaojitambulisha kuwa wamiliki halali wa eneo hilo maarufu kama SOMJI; wananchi katika hatua mbalimbali wamepeleka malalamiko Serikalini kuanzia ngazi ya Wilaya, Wizara ya Ardhi na hata kwa Waziri Mkuu lakini mpaka sasa hakuna utatuzi uliofanyika.
Je, hatua gani zimeanza kuchukuliwa ili kero hiyo ya muda mrefu imalizike?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali namba 17 la Mheshimiwa Halima Mdee, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, awali shamba hili lililokuwa na ukubwa wa ekari 366 Mbweni maarufu kama Somji Farm lilipimwa na upimaji namba E7/37F na kupewa namba ya upimaji 10,917 ya tarehe 15 Agosti, 1959. Baada ya upimaji shamba lilimilikishwa kwa Ndugu Hussein Somji pamoja na Ndugu Munaver Somji mwaka 1961 na baadae kuandaliwa hati iliyosajiliwa kwa namba 14,573 ya kipindi cha miaka 99.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya shamba hilo, ekari 5.8 zilitwaliwa kwa matumizi mahususi ya Serikali mwaka 1975 na kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali Namba 670 la tarehe 30 Mei, 1975. Aidha, sehemu iliyobaki yenye ekari 357.5 ilitwaliwa na Serikali tena mwaka 2002 na kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali Namba 617 la tarehe 27, Septemba, 2002 kwa ajili ya kutumika katika mradi wa viwanja 20,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo eneo hilo halikuingizwa kwenye mradi kutokana na sehemu kubwa kuwa imevamiwa na wananchi. Pamoja na uvamizi huo, wamiliki wa awali walifungua mashauri mahakamani dhidi ya Serikali kupinga eneo lao kutwaliwa; shauri la Kikatiba namba moja la 2003 na shauri la Kikatiba namba 40 la 2010. Uwepo wa mashauri haya ulikwamisha juhudi za Serikali kushughulikia mgogoro huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kwa kushirikiana na Manispaa ya Kinondoni mara kadhaa imekaa na wahusika kwa lengo la kuweka utaratibu utakaowezesha wamiliki wa awali kulipwa fidia stahiki kwa fedha iliyopatikana kutokana na wanachi ambao watatakiwa kurasimishiwa maeneo waliyojenga.
Hata hivyo changamoto iliyopo ni katika kumilikisha makubaliano haya kwa wananchi kupitia kamati yao waliyounda, kutokuwa tayari kuchangia gharama za kurasimisha eneo hilo. Jitihada zaidi za wadau wengine akiwemo Mbunge zinahitajika katika kuwaelimisha wananchi kupitia Kamati yao kuwa tayari kushiriki katika upatikanaji wa ufumbuzi wa suala hili.