Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 9 Good Governance Ofisi ya Rais TAMISEMI. 111 2018-02-09

Name

Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Primary Question

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:-
Je, ni lini Mfumo wa EPICOR, LGMD na ule wa LAWSON iliyopo kwenye halmashauri itaanza kuwasiliana na si kuwa stand alone system kama ilivyo sasa?

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo hii; ule wa Usimamizi wa Fedha za Umma (Intergrated Financial Management Systems – IFMS) au EPICOR, Mfumo Shirikishi wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (Human Capital Management Information System) au Lawson na Mfumo wa Ukusanyaji Takwimu za Utoaji Huduma (Local Government Monitoring Database) ilinunuliwa kwa nyakati tofauti kutegemeana na teknolojia iliyokuwepo wakati huo na kwa madhumuni tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na teknolojia zake, ni kweli mifumo hiyo ilikuwa haiingiliani au kubadilishana taarifa (automatic data exchange). Hali hii imesababisha kuwepo kwa changamoto ya kuongezeka kwa gharama za uendeshaji na usimamizi. Gharama hizi ni pamoja na mafunzo kwa watumiaji, leseni za mifumo, ununuzi wa mitambo na vifaa pamoja na gharama nyingine za uendeshaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuhakikisha kuwa mifumo hii inaunganishwa ili kuleta ufanisi na kupunguza gharama za uendeshaji kwa kuwa sasa teknolojia imekuwa na pia uwezo wa Serikali kiutaalam umeongezeka hususan baada ya kuanzisha Wakala wa Serikali Mtandao (eGA) na Idara/ Vitengo vya TEHAMA katika Ofisi za Serikali kuanzia miaka ya 2010.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha kuwa mifumo hii inawasiliana hatua zifuatazo zimechukuliwa:-
(a) Kuandaa miongozo ya viwango (technical specifications) kwa kuzingatiwa wakati wa kusanifu, kujenga na kuimarisha au kuhuisha mifumo kwa lengo la kufanya maandalizi ya kuunganisha na kuimarisha.
(b) Kutengeneza mfumo maalum wa ubadilishanaji taarifa kutoka mifumo mbalimbali.
(c) Kuweka miundombinu ya TEHAMA ambapo mtandao mkuu wa mawasiliano Serikalini ambapo taasisi, tumeziorodhesha 72 za Serikali, Wizara 26, Wakala wa Serikali 29, Idara zinazojitemea 17 zilizopo Dar es Salaam, Dodoma na Pwani. Aidha, Serikali imeunganisha katika mtandao huu taasisi za Serikali zilizopo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa 77, Sekretarieti za Mikoa 20, Halmashauri za Majiji, Miji, Wilaya 38 na Hospitali za Mikoa 19 kwa lengo la kuwezesha kuunganisha mifumo inayotumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba kulingana na mpango kazi uliopo kazi iliyobaki ya kuunganisha mifumo mbalimbali ndani ya Serikali, ikiwemo mifumo hii mikuu inatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2019/2020.