Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 8 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 101 2018-02-08

Name

Mwantum Dau Haji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-
Kumekuwa na sintofahamu ya matumizi ya ardhi pamoja na masharti maalum yanayotakiwa katika mapori yetu hususan kwa wawekezaji na wananchi wanaozunguka hifadhi na mapori tengefu.
Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza tatizo hili?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya hifadhi na mapori tengefu yametengwa kwa mujibu wa Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009.
Aidha, uwekezaji katika hifadhi, mapori ya akiba na tengefu, maeneo ya wazi yenye wanyamapori, maeneo ya Jumuiya ya Hifadhi na Wanyamapori (WMAs) husimamiwa na sheria hiyo. Sheria na Kanuni husika hutoa taratibu za usimamizi wa maeneo hayo muhimu kwa maslahi ya uhifadhi, maliasili na mazingira, ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi kupitia matumizi endelevu. Mwekezaji anapaswa kupata kibali na leseni ya kumruhusu kuendesha shughuli za utalii kutoka mamlaka zinazohusika kabla ya kuanza biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na tatizo hilo Serikali inapitia upya kanuni na taratibu za uwekezaji katika maeneo ya hifadhi na mapori tengefu, miongoni mwa kanuni zinazopitiwa ni pamoja na Kanuni ya Jumuiya za Hifadhi Wanyamapori (WMAs).
Aidha, Serikali iko katika hatua za mwisho katika maandalizi ya kanuni za maeneo ya mapito (shoroba) ya wanyama na mtawanyiko wa wanyamapori.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara itaendelea kutoa elimu kwa wawekezaji na wananchi wanaozunguka maeneo yaliyohifadhiwa. Aidha, natoa wito kwa wawekezaji kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo ili kuepukana na migogoro ya ardhi baina ya wanavijiji, wawekezaji na Mamlaka za Hifadhi.