Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 7 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 87 2018-02-07

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Kumekuwa na mgogoro wa mipaka katika Pori la Hifadhi ya North Ugala, Wilayani Urambo, Kata ya Nsenda, Kijiji cha Kangome, Kitongoji cha Lunyeta. Mgogoro huo umesababishwa na mipaka mipya iliyowekwa na hivyo kusababisha upungufu wa eneo la shughuli za kilimo na ufugaji.
(a) Je, Serikali inafahamu kuwepo wa mipaka ya zamani ambayo haikuzingatiwa wakati wa kuweka mipaka mipya?
(b) Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa mipaka ili wananchi wapate eneo la kutosha kwa ajili ya kilimo na ufugaji?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo lenye sehemu
(a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu wa Hifadhi ya North Ugala unapatikana katika Wilaya za Urambo na Kaliua. Msitu huu unaomilikiwa na Serikali Kuu chini ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania na una ukubwa wa hekta 163,482.39 na ulianzishwa rasmi 1956 na kuchorewa ramani ya JB Namba 307 ya tarehe 22/10/1956.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu wa North Ugala umehifadhiwa kutokana na umuhimu wake hasa katika kuhifadhi vyanzo vya maji, mapito (shoroba) za wanyamapori hasa wanapohama kutoka katika Mapori ya Akiba ya Kigosi, Ugala na Rungwa kuelekea Pori la Akiba la Rukwa, Lukwati hadi Hifadhi ya Taifa ya Katavi iliyopo Mkoani Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, hifadhi hii inatumika katika uzalishaji na uvunaji wa mazao ya misitu ikiwemo asali, nta, mbao na mkaa. Serikali iliagiza kuweka vigingi kwenye mipaka yote ya Hifadhi za Taifa, misitu, mapori ya akiba na tengefu. Katika hifadhi ya msitu wa North Ugala, vigingi viliwekwa na baadae kuwaondoa wananchi wote waliokuwa wamevamia hifadhi hiyo. Baada ya kupitia na kuweka vigingi katika mpaka, ilionekana kwamba mpaka umenyooka kutoka kigingi namba 5 hadi 6 na kupitia katika mpaka wa vijiji vya Izengabatogilwe, Isongwa, Azimio, Mtakuja, Ifuta, Utenge, Tumaini, Kamalendi, Igombe, Zugimlole na Uyumbu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mpaka mpya uliowekwa bali vigingi viliwekwa kwa mujibu wa GN iliyounda hifadhi hiyo. Ili kumaliza migogoro kati ya hifadhi na wananchi wanaopakana na hifadhi ya misitu; Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa misitu, ushirikishwaji wa wananchi katika uhifadhi, kuimarisha mipaka kwa kuweka vigingi na mabango ya tahadhari, kupanda miti mipakani, kushirikiana na sekta nyingine katika kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi na kuhamasisha ufugaji na kilimo cha kisasa. (Makofi)