Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 32 2018-02-01

Name

Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Upembuzi yakinifu wa kutumia chanzo cha maji cha Mto Ibofwe ili kumaliza tatizo la maji katika Kata za Magulilwa, Luhota, Mseke, Ifunda, Mgama na Maboga ulifanyika kati ya mwaka 1995 – 2000 chini ya usimamizi wa Mbunge wakati huo, Mheshimiwa George Mlawa na bajeti ya utekelezaji wake kupitishwa na Bunge hili ili uwe katika kipindi cha mwaka 2000-2005/2005-2010.
Je, ni tatizo gani lililofanya mradi huo usikamilike na kuwaacha wananchi wakiendelea kuteseka wakati Bunge lilikwishapitisha bajeti ya mradi?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji wa kutumia chanzo cha Mto Ibofwe ulifanyiwa usanifu wa awali miaka ya 1990 lakini haukufanyiwa usanifu wa kina (detailed design) ambao ungebaini mahitaji na gharama halisi za kutengeneza mradi huo ndiyo maana haukutekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwapatia huduma ya maji wananchi wa Kata za Maboga, Lumuli, Isupilo na Itengulinyi, Serikali inatekeleza mradi mkubwa wa maji unaogharimu shilingi bilioni 2.18 utakaonufaisha wakazi 6,914 katika maeneo hayo. Mradi huo ulioanza kutekelezwa mwaka 2013/2014 ulisimama utekelezaji wake mwaka 2015 kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 umetengewa shilingi milioni 800 na unatarajiwa kukamilika Desemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kati ya Julai 2016 na Desemba 2017, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo imechimba visima sita katika Kata za Magulilo kisima kimoja, Luhota visima vitatu, Maboga kisima kimoja na Mgama kisima kimoja vinavyohudumia wananchi 1,600. Idadi ya visima kwenye kata hizo tangu miaka ya 1990 hadi sasa imefikia visima 41 vinavyohudumia wakazi 8,200.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mwaka huu 2017/2018, jumla ya shilingi 410,000,000 zimetengwa kutekeleza miradi ya maji ya Izazi - Mnadani, Migoli - Mtera, Malinzanga, Isupilo – Lumweli – Itengulinyi - Magunga na Mfyome. Mpango wa muda mrefu wa Serikali ni kufanya usanifu wa kina (detailed design) ili hatimaye tutumie chanzo cha Mto Ibofwe kumaliza kabisa matatizo ya maji kwenye maeneo hayo. Usanifu wa kina utafanyika mwaka 2018/2019 kwa gharama ya shilingi milioni 49.56 ambazo ziko kwenye mapendekezo ya bajeti ya mwaka 2018/2019 endapo Bunge litaridhia.