Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 31 2018-02-01

Name

Martha Jachi Umbulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-
Hospitali ya Rufaa ngazi ya Mkoa ya Haydom inahudumia wananchi wengi lakini inakabiliwa na changamoto ya uhaba wa watumishi, madaktari wakiwemo Madaktari Bingwa pamoja na ukosefu wa maji.
(a) Je, Serikali itachukua hatua gani za dharura kutatua changamoto hizo?
(b) Kwa kuwa watumishi hawa wanafanya kazi katika mazingira magumu, je, ni kwa nini Serikali isiondoe kodi kwenye posho zao kama vile on-call allowance, hardship allowance na food allowance?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Haydom inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) ina jumla ya watumishi 680 ambapo kati yao watumishi wa Serikali ni 156. Serikali imekuwa ikiisaidia hospitali kupitia Sera ya Ushirikiano kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP) ambapo mpaka sasa imepeleka watumishi 156 wa kada mbalimbali wakiwepo madaktari 10 ambapo saba ni Madaktari Bingwa na watatu ni Madaktari wa Kawaida. Mbali na watumishi, Hospitali ya Haydom inapata ruzuku ya dawa kupitia MSD na ruzuku ya fedha za Busket Funds kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu. Hata hivyo, Serikali itaendelea kupeleka watumishi hasa madaktari na wauguzi kadri vibali vya ajira vitakavyokuwa vinapatikana.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Haydom inapata maji kutoka chanzo cha maji kilichopo umbali wa kilometa 20 katika Kijiji cha Binja, Kata ya Endamilay, Wilaya ya Mbulu. Hospitali hiyo inajitosheleza kabisa kwa maji hayo. Hata hivyo, maji haya yanapatikana kwa gharama kubwa kutokana na kukosekana kwa nishati ya umeme katika eneo husika, hivyo hospitali kulazimika kusukuma maji kwa kutumia mitambo ya dizeli (jenereta) inayotumia jumla ya lita 2,800 kwa mwezi sawa na shilingi 6,020,000/= ambayo ni sawa na shilingi 72,240,000/= kwa mwaka.
Kwa kuwa hivi sasa kupitia Mradi wa Usambazaji Umeme Vijijini (REA) inasambaza umeme katika maeneo mbalimbali yakiwapo ya Haydom inatarajiwa kuwa umeme huo utasaidia mradi wa maji wa Hospitali ya Haydom kupata huduma ya umeme na hivyo kupunguza gharama za uendeshaji wa kutumia dizeli.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Haydom ina makundi mawili ya waajiriwa kama ifuatavyo; kundi la kwanza ni waajiriwa walioajiriwa na Hospitali ya Haydom moja kwa moja na hukatwa kodi ya mapato kama sheria inavyoelekeza; kundi la pili ni la waajiriwa waliajiriwa na Serikali lakini wanafanyakazi Hospitali ya Kilutheri Haydom, watumishi hawa wanalipwa posho ya kuitwa kazini baada ya masaa ya kazi (on-call allowance) na Hospitali ya Haydom na hii ndiyo sababu inayopelekea wakatwe kodi katika posho hiyo. Makato hayo yanatokana na Sheria ya Kodi ya Mapato (Income Tax) ya mwaka 1973.