Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 17 2018-01-31

Name

Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:-
Halmashauri zina wataalam wa kusimamia na kutekeleza mipango yao na zina uwezo kisheria kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo, elimu, afya, maji kilimo na ardhi pasipo kuingiliwa. Viongozi na Watendaji wa Serikali ngazi za Mkoa na Wilaya huambiwa watawajibishwa kufikia malengo mathalani, katika ujenzi wa maabara, madarasa na kutengeneza madawati:-
Je, mipaka ipi ni ya kinadharia (theoretical) na ipi inatekeleza (practical) kiutendaji na uwajibikaji kati ya viongozi wa Serikali Kuu na Halmashauri za Majiji, Miji na Wilaya?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Joseph Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ugatuzi wa madaraka ya kisiasa, fedha na utawala kutoka Serikali Kuu kwenda kwa wananchi kupitia Serikali za Mitaa umetokana na mahitaji ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 145 na 146. Madhumuni ya ugatuzi ni kuwapa wananchi kupitia Mabaraza yao ya Madiwani, uwezo wa kufanya maamuzi kulingana na mahitaji yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali za Mitaa zimeundwa kwa mujibu wa Sheria Na.7 (Mamlaka za Wilaya) na Sheria Na.8 (Mamlaka za Miji)kwa malengo ya kuboresha na kuimarisha utoaji wa huduma mbalimbali za jamii kwa wananchi pamoja na kusimamia ulinzi na usalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na sheria kuweka utaratibu wa Serikali za Mitaa kujiamulia mambo yake kupitia vikao rasmi, hazijapewa uwezo wa kukataa maelekezo ya Serikali Kuu. Kwa mujibu wa Sera ya Maboresho ya Serikali za Mitaa ya Mwaka 1998, Serikali Kuu ina majukumu ya kutunga sera, kutoa miongozo ya namna bora ya kutekeleza sera, kuandaa mikakati ya kitaifa, kuweka mazingira bora ya utekelezaji wa sera kwa kuzipatia Serikali za Mitaa rasilimali watu, rasilimali fedha na baadhi ya vitendea kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuweka viwango vya utekelezaji, kufuatilia utekelezaji ili kujiridhisha kuwa miongozo na viwango vinazingatiwa na kuchukua hatua dhidi ya utekelezaji usioridhisha inapobidi hasa inapobainika matumizi yasiyo sahihi ya fedha ikiwemo viwango duni vya miradi visivyolingana na thamani ya fedha iliyotumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali Kuu huwakilishwa na viongozi wa Mikoa na Wilaya katika kusimamia utekelezaji wa sera na miongozo, Viongozi Wakuu wa Serikali ngazi ya Mikoa na Wilaya hutekeleza majukumu yao ya kisheria ya kuziwezesha Serikali za Mitaa kutimiza majukumu yao kikamilifu ikiwemo kutekeleza maagizo halali na ushauri wa viongozi hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikibainika kiongozi wa Mkoa au Wilaya ameshindwa kutimiza wajibu wake na hivyo kusababisha Mamlaka ya Serikali za Mtaa zisitimize vizuri majukumu yao, Mamlaka ya uteuzi huchukua hatua za kiutawala. Napenda kusisitiza kwamba Katiba, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo ya Utumishi zikirejewa vizuri hakuna mgogoro wowote wa kimipaka wala kiutendaji utakaodhihiri.