Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 1 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 03 2018-01-30

Name

Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Primary Question

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI aliuliza:-
Wilaya ya Namtumbo haina huduma stahiki za Hospitali ya Wilaya wala Vituo vya Afya licha ya kuwepo kwa Sera ya kila Wilaya iwe na Hospitali ya Wilaya na kila Kata iwe na Kituo cha Afya.
(a) Je, sera hiyo kwa Wilaya ya Namtumbo itatekelezwa lini?
(b) Makadirio yaliyofanywa na TBA kwa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Namtumbo ni shilingi bilioni19. Je, Serikali ipo tayari kutenga na kutoa kiasi hicho katika bajeti ya mwaka 2018/2019?
(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa vitendea kazi na wataalam katika Vituo vya Afya vitano vilivyopo Namtumbo ili viweze kutoa huduma bora za afya?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Amandus Ngonyani, Mbunge wa Namtumbo, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Namtumbo ulianza rasmi mwaka 2010 na unatekelezwa kwa awamu tofauti ambapo mpaka sasa unaendelea. Aidha, kiasi cha shilingi milioni 600 kimeshatumika kwa ajIli ya kujenga majengo ya utawala, jengo la wagonjwa wa nje yaani OPD, chumba cha kujifungulia yaani labour room, kichomea taka (incinerator), msingi na jamvi kwa chumba cha akina mama wajawazito (maternity ward) pamoja na mfumo wa maji safi na taka (water and sewage system). Kwa mwaka 2017/2018, Halmashauri imepokea shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuendeleza na kumaliza jengo la wodi ya akina mama wajawazito.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo la upasuaji ili kuimarisha huduma za upasuaji katika hospitali hiyo.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Namtumbo ina jumla ya vituo vya afya saba ambapo vitano vinamilikiwa na Serikali na viwili vinamilikiwa na mashirika ya dini. Vituo vya Afya vya Serikali ni Namtumbo, Msindo, Mputa, Mkongo na Lusewa. Vituo vya Afya vya mashirika ya dini ni Namabengo na Hanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, huduma ya upasuaji wa dharura kwa akinamama wajawazito inafanyika katika Kituo cha Afya Hanga. Katika Kituo cha Afya Lusewa, jengo la upasuaji lipo katika hatua za mwisho za ukamilishaji na vifaa vya upasuaji vipo katika mchakato wa kununuliwa lakini kuna tatizo la maji ambalo pia linashughulikiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Namtumbo kimepokea jumla ya shilingi milioni 400 tarehe 21 Desemba, 2017 kwa ajili ya ujenzi, ukarabati wa majengo ya upasuaji, wodi ya wazazi, maabara na chumba cha kuhifadhia maiti ambayo kazi yake inaendelea katika hatua za ukamilishaji na inategemea kukamilika tarehe 30 Aprili,2018. Aidha, Serikali imeagiza vifaa vya chumba cha upasuaji kwa ajili ya kutoa huduma ya upasuaji kwa akina mama wajawazito (CeMOC) kwa Vituo vya Afya vya Msindo na Mputa ili kuondoa tatizo la vifo vitokanavyo na uzazi.