Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 9 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 117 2017-11-17

Name

Halima Abdallah Bulembo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HALIMA A. BULEMBO aliuliza:-
Kumekuwa na upandaji holela wa gharama za pango kwa nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).
Je, Serikali haioni kwamba kuna haja ya kudhibiti upandaji holela wa pango ambao unaathiri wananchi wengi kutokana na kipato chao?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima Abdallah Bulembo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Nyumba la Taifa linaendeshwa kwa mujibu wa sheria, taratibu na miongozo ya Serikali. Aidha, masuala ya upingaji wa kodi huongozwa na Sheria ya Ardhi namba 4 ya mwaka 1999 na sheria iliyoanzisha Shirika la Nyumba la Taifa Na. 2 ya mwaka 1990 kama zilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2005. Sheria zote mbili zimeweka viwango ambavyo mmiliki wa nyumba ikiwemo Shirika la Nyumba la Taifa anapaswa kuzingatia katika ukadiriaji wa kodi za pango. Miongoni mwa vigezo hivyo ni ukubwa wa nyumba, mahali nyumba ilipo, hali ya nyumba na kodi za Serikali zinazolipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa kurekebisha viwango vya kodi ya nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa husimamiwa na bodi ya wakurugenzi ambayo imepewa mamlaka ya kisheria ya kusimamia kodi ya pango pamoja na kuidhinisha viwango vya kodi vitanavyotozwa kwa wapangaji wa nyumba za Shirika la Nyumba. Tangu mwaka 1990 shirika limefanya marekebisho ya kodi kwa miaka 6; 1994, 1999, 2001, 2005, 2007, 2008 na 2011.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na marekebisho hayo, bado viwango vya kodi ya pango kwa nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa ni kati ya asilimia 42 hadi 80 ya viwango vya soko. Kwa mfano, eneo la Masaki Shirika la Nyumba la Taifa hutoza kodi ya shilingi 1,700 kwa kila mita ya mraba wakati bei ya soko katika eneo hilo ni kati ya shilingi 12,000 hadi 30,000 kwa mita mraba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara ya mwisho Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Nyumba la Taifa iliidhinisha viwango vipya kwa kutoza kodi kwenye nyumba za shirika mwaka 2011 ambavyo ndivyo vinatumika mpaka sasa. Utaratibu wa kupandisha kodi kwa sasa hufanyika pale mkataba wa mpangaji unapomalizika na mpangaji kuomba kuhuisha mkataba wake. Ieleweke kuwa kodi zinapanda kwa mujibu wa sheria na pale mkataba wa mpangaji unapomaliza muda wake.