Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 9 | Sitting 6 | Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives | Wizara ya Mifugo na Uvuvi | 80 | 2017-11-14 |
Name
Mashimba Mashauri Ndaki
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Maswa Magharibi
Primary Question
MHE. MASHIMBA M. NDAKI aliuliza:-
Shamba la malisho lililopo katika Kata ya Shishiyu Wilayani Maswa linamilikiwa na Serikali lakini halitumiki ipasavyo:-
Je, Serikali Kuu haioni haja ya kulirejesha shamba hilo kwa Halmashauri ya Wilaya ili lipangiwe matumizi mengine?
Name
Abdallah Hamis Ulega
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mkuranga
Answer
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha kupumzishia mifugo (holding ground) cha Shishiyu kina ukubwa wa hekta 4,144 na ni kati ya vituo 28 vilivyotengwa nchi nzima kwa mujibu wa Sheria ya Magonjwa ya Wanyama Na. 17 ya mwaka 2003 kwa ajili ya kukusanya na kupumzisha mifugo inayotoka minada mbalimbali kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa kabla ya kusafirisha mifugo hiyo kwenda katika viwanda vya kuchinja na kuchakata nyama au kusafirisha kwenda nje ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, uwepo wa vituo vya kupumzishia mifugo ni hitaji la Kimataifa katika biashara ya mifugo. Zipo sheria mbalimbali za Kimataifa zinazolazimisha uwepo wa maeneo haya, yanayolenga utoaji huduma unaozingatia viwango ambazo zinasimamiwa na Shirika la Afya ya Wanyama ulimwenguni - OIE na makubaliano ya Kimataifa ya afya ya wanyama na mimea (Sanitary and Phytosanitary (SPS) chini ya Shirika la biashara la Kimataifa (WTO).
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili pia hutumika kama kituo cha karantini kwa ajili ya kuchunguza magonjwa, hususan yale ya milipuko yanapojitokeza hasa kutokana na Kanda ya Ziwa kuwa na mifugo mingi na baadhi ya mikoa katika Kanda hii inapakana na nchi jirani hivyo ni rahisi ka magonjwa ya wanyama ya milipuko kujitokeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kuna mwingiliano mkubwa wa wanyama wafugwao na wanyama pori kutoka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Pori Tengefu la Maswa kutokana na umuhimu wa kituo hiki kwa ajili ya biashara ya mifugo ndani na nje ya nchi. Hivyo, siyo vema kubadilisha matumizi na madhumuni ya kuanzishwa kwa kituo hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, eneo hili litaendelea kubaki chini ya usimamizi wa Serikali Kuu kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili eneo hili liweze kutumiwa na wadau wote waliopo kwenye mnyororo wa kuongeza thamani (value chain) ya mifugo na mazao yake.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved