Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 70 2017-11-14

Name

Josephine Tabitha Chagulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE T. CHAGULA aliuliza:-
Hospitali ya Mkoa wa Geita inakabiliwa na kero mbalimbali kama vile ukosefu wa Madaktari Bingwa wa akinamama na watoto, dawa, vifaa tiba pamoja na uhaba wa majengo ya wodi za wazazi:-
Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kutatua kero hizo katika Hospitali ya Mkoa wa Geita?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:- Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tabitha, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mkoa wa Geita ina Daktari Bingwa mmoja wa upasuaji. Madaktari wengine watatu wako masomoni akiwemo Daktari Bingwa wa Magonjwa ya akina Mama na Watoto. Ukosefu wa Madaktari Bingwa unasababishwa na uchache wa Madaktari ukilinganisha na uhitaji wetu. Katika kibali cha mwaka wa fedha 2017/2018 cha kuajiri watumishi 2,058 kilichokuwa na Madaktari 46, Hospitali ya Mkoa wa Geita imepangiwa jumla ya Madaktari wanne ambao wamesharipoti na wameanza kazi, naamini Madaktari hao watapunguza uhaba uliopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa dawa, Mkoa wa Geita umepanga kuanzisha duka la dawa kwa kutumia mkopo wa shilingi milioni 160 kutoka NHIF. Wagonjwa watapatiwa dawa na vifaa tiba kwa gharama nafuu zaidi ili kuwa na uhakika wa upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kwa wagonjwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika kutatua tatizo la uhaba wa miundombinu mkoa unaendelea na ujenzi wa Hospitali Mpya ya Rufaa ya Mkoa wa Geita. Ujenzi upo katika hatua za msingi kwa majengo manne ambayo ni jengo la upasuaji, wagonjwa wa nje, jengo la mionzi na jengo la kufulia nguo. Kazi hii inatekelezwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).