Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Energy and Minerals Wizara ya Madini 50 2017-11-10

Name

Njalu Daudi Silanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Itilima

Primary Question

MHE. KISWAGA B. DESTERY (K.n.y. MHE. NJALU D. SILANGA) aliuliza:-
Maeneo mengi yamefanyiwa utafiti na kampuni za kigeni kwa muda mrefu bila kufikia hatua ya kufungua migodi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuzifutia leseni kampuni hizo na kuwapatia wachimbaji wadogo wadogo?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza kabisa na mimi kwa sababu nimesimama hapa kwa mara yangu ya kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii kufika hapa leo. Vilevile nimshukuru pia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kuniamini na kuniweka katika Wizara hii mpya. Vilevile nimshukuru Mheshimiwa Spika, Wabunge wote na Wajumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara kwa malezi yao mazuri na kunifikisha hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Njalu Daudi Silanga lililoulizwa na Mheshimiwa Kiswaga ambaye ni Mbunge wa Magu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na kanuni zake inatambua umiliki wa leseni za utafutaji mkubwa wa madini na uchimbaji mdogo wa madini inayotolewa kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kama ilivyorekebishwa mwaka 2017, leseni za utafutaji wa madini aina ya metali, viwandani na nishati (makaa ya mawe na urani) hutolewa kwa muda wa miaka minne ya awali na kuhuishwa kwa mara ya kwanza kwa miaka mitatu na mara ya pili kwa miaka miwili. Hivyo leseni ya utafutaji mkubwa wa madini ya aina hizo hubaki hai kwa kipindi cha miaka tisa. Aidha, leseni za utafutaji wa madini na vito na ujenzi hutolewa kwa mwaka mmoja na haziwezi kuhuishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo mmiliki wa leseni atashindwa kuendesha shughuli za utafutaji wa madini, leseni yake hufutwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na Marekebisho yake ya mwaka 2017. Aidha, katika kipindi cha mwaka 2014/2015 hadi 2016/2017 jumla ya leseni 423 za utafutaji wa madini zilifutwa ambapo mwaka 2014/ 2015 zilifutwa leseni 2013, mwaka 2015/2016 zilifutwa leseni 155 na mwaka 2016/2017 zilifutwa leseni 65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la leseni lililofutwa hutathminiwa na Wakala wa Jiolojia yaani Geological Survey of Tanzania (GST) kwa ajili ya kutengwa kwa wachimbaji wadogo endapo litaonekana kuwa na mashapo yenye tija. Katika kipindi cha mwaka 2014/2015 hadi 2016/2017 jumla ya maeneo 19 yenye ukubwa wa jumla takriban hekta 69,652.88 yalitengwa kwa wachimbaji wadogo katika maeneo mbalimbali nchini.
Aidha, Serikali itaendelea kufuatilia na kujadiliana na kampuni zilizomiliki leseni za utafutaji wa madini ili kuona uwezekano wa kuachia baadhi ya maeneo yanayofaa kwa uchimbaji mdogo.