Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 48 2017-11-10

Name

Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Primary Question

MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-
Katika Wilaya ya Mbogwe kuna Kitalu cha Kigosi North kilichopo katika Pori la Akiba la Kigosi.
(a) Je, ni lini Serikali itaanza kulipa Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe asilimia 25 ya ada ya uwindaji?
(b) Je, ni lini Serikali italitengeneza greda lililoko Kifura Kibondo Makao Makuu ya Mapori ya Kigosi Moyowosi ili lisaidie matengenezo ya barabara ndani ya mapori haya?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imekuwa na utaratibu wa kutoa fedha kiasi cha asilimia 25 kwenye Halmashauri za Wilaya zinatokana na malipo ya ada ya wanyamapori (game fees) wanazowinda kwenye maeneo yanayopakana na Wilaya husika kwa ajili ya kusaidia shughuli za maendeleo na uhifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitalu cha Kigosi North kimekuwa kikitumika kwa ajili ya utafiti wa madini uliokuwa unafanywa na Kampuni ya TANZAM na siyo kwa shughuli za uwindaji wa kitalii. Hali hiyo inafanya Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe isipate fedha za asilimia 25 kwa ajili ya uwindaji wa kitalii katika kitalu hicho. Kitalu cha Kigosi East ndiyo kitalu kilichotengwa kwa shughuli za uwindaji wa kitalii kwa kipindi cha mwaka 2013 hadi 2018. Hata hivyo, mwekezaji katika kitalu hicho amejaribu kuleta wageni mara mbili mwaka 2013 na 2014 kwa ajili ya kuwinda lakini hakuweza kuwinda kutokana na kuwepo kwa ng’ombe wengi badala ya wanyamapori katika kitalu hicho. Kwa sababu hiyo, hakuna wanyamapori waliowindwa kwa kipindi cha mwaka 2013 hadi 2016 kutokana na kuwepo kwa ng’ombe na hivyo kitalu husika kurudishwa Serikalini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na jitahada za Serikali za kuondoa mifugo katika maeneo yote ya hifadhi, ni wazi kuwa mazingira ya asili pamoja na wanyamapori watarejea na hivyo kuwezesha kitalu hicho kutumika kwa uwindaji wa kitalii kuanza kufanyika. Kufanyika kwa uwindaji wa kitalii katika kitalu hicho kutawezesha upatikanaji wa fedha ambazo zitaweza kuanza kuwasilishwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe. Wizara yangu inatoa wito kwa Wilaya zote zenye uvamizi wa mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa kuhakikisha mifugo inaondolewa ili kurejesha hadhi ya vitalu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kutengeneza greda, Wizara yangu tayari imeshatengeneza greda lililopo Kifura katika Pori la Akiba Moyowosi Kigosi na sasa linafanya kazi.