Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 36 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 293 2017-05-29

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:-
Mgodi wa GGM - Geita umekuwa ukitumia milipuko mikubwa wakati wa kulipua miamba ya dhahabu na kusababisha madhara makubwa kwa wananchi jirani na maeneo hayo, kama wale wa eneo la Katoma.
• Je, Serikali inafahamu kwamba nyumba za wananchi zinapasuka na baadhi ya watu huzimia kutokana na mshtuko?
• Je, Serikali inalitatua vipi tatizo hilo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tangu shughuli za ulipuaji zianze katika eneo la Katoma tarehe 23 Septemba, 2014 kumekuwepo na malalamiko kutoka kwa wananchi wa kijiji hicho kuwa milipuko inayofanywa na Kampuni ya GGM imekuwa ikisababisha sauti na mitetemo mikubwa na hivyo kuleta usumbufu na athari mbalimbali kwa wananchi na majengo yao.
Mheshimiwa Spika, kufuatia malalamiko hayo, mwaka 2014 Serikali kupitia Idara ya Madini na Halmashauri ya Wilaya ya Geita kwa kushirikiana na wananchi wa Mtaa wa Katoma pamoja Geita GGM, waliunda Kamati shirikishi ya kushughulikia malalamiko ya wananchi hao, ijulikanayo kama Blast Monitoring Committee (BMC). Kazi kubwa ya Kamati hiyo ilikuwa ni kukutana kila siku ya ulipuaji na kupokea malalamiko wakati wa mlipuko.
Mheshimiwa Spika, mwezi Machi, 2016 Wizara ilituma timu ya wataalam kutoka Wakala wa Jiolojia Tanzania – GST kwa ajili ya kufanya tathmini ya kina ya nyufa za nyumba ambazo zimesababishwa na GGM. Timu hiyo ilibaini uwezekano wa milipuko ya mgodi huo katika shimo la Katoma kuchangia nyufa katika nyumba na maeneo mengine ya Katoma pamoja na Nyamalembo Compound.
Mheshimiwa Spika, kutokana na taarifa hiyo ya GST, Wizara iliunda timu ya wataalam iliyojumuisha wawakilishi wa wananchi wa maeneo hayo ili kufanya utambuzi wa nyuma zenye nyufa. Kutokana na utambuzi huo, takribani nyumba 890 katika maeneo hayo zilibainika kuwa na nyufa. Hivi sasa uchambuzi wa kina unafanywa kuhusiana na hatua stahiki za kuchukua uchambuzi huo utatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2017 na taarifa yake itatolewa kwa wananchi.