Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 35 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 280 2017-05-26

Name

Njalu Daudi Silanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Itilima

Primary Question

MHE. MASHIMBA M. NDAKI (K.n.y. MHE. NJALU D. SILANGA) aliuliza:-
Wilaya ya Itilima ni mpya na ina eneo kubwa linalovutia kwa ajili ya makazi na shughuli za kilimo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuunganisha miundombinu ya barabara ya Migato, Nkuyu, Longalombogo, Laini, Bulombeshi na Bumera ili kuvutia watu kufanya biashara za mazao katika maeneo hayo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njalu Daudi Silanga, Mbunge wa Jimbo la Itilima, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuunganisha maeneo ya Migato, Nkuyu, Longolombogo, Laini na Bulombeshi kwa uboreshaji wa mtandao wa barabara kama ifuatavyo:-
Barabara ya Bumera - Bulombeshi na Bumera - Gaswa - Sagata - Laini ya kilometa 20, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 imefanyiwa matengenezo ya sehemu korofi kwa kunyanyua tuta na kuweka changarawe kilometa 3 na kujenga Kalavati 9 katika barabara ya Bulombeshi – Bumera - Gaswa. Katika bajeti ya mwaka 2017/2018 zimetengwa shilingi milioni 99.6 kwa ajili ya matengenezo ya muda maalum urefu wa kilometa sita na matengenezo ya kawaida urefu wa kilometa nane katika barabara ya Bumera - Gaswa - Laini.
Barabara ya Migato - Ndoleleji - Nkuyu yenye kilometa 22.9, mwaka wa fedha 2016/2017 imefanyiwa matengenezo katika maeneo korofi kwa kiwango cha changarawe na kujenga makalvati matatu katika barabara ya Migato - Ndoleleji yenye urefu wa kilometa 6.5.
Lagangabilili - Muhuze - Migato mpaka unapofika Longolombogo yenye kilometa 40, kwa mwaka wa fedha 2015/2016 barabara hiyo imefanyiwa matengenezo katika kipande cha Lagangabilili - Muhuze - Migato kilometa 11 na kujenga makalvati kumi. Katika bajeti ya 2016/2017 yamejengwa makalvati sita na kuwekwa changarawe baadhi ya maeneo korofi yenye urefu wa kilometa 15. Aidha, katika bajeti ya 2017/2018, jumla ya shilingi milioni 49.18 zimetengwa kwa ajili ya kufanya matengenezo mbalimbali katika barabara hii.