Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 8 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 104 2017-09-14

Name

Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Kigoma Mjini

Primary Question

MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y MHE. KABWE Z. R. ZITTO) aliuliza:-
Nchi ya DRC inaitegemea Kigoma kiuchumi kwa kiwango kikubwa hususan katika soko la bidhaa na huduma ya bandari ya Kigoma na hivyo wananchi wengi wa Kigoma kutembelea Congo na wale wa Congo kutembelea Kigoma. Changamoto kubwa ni gharama za biashara kutokana na viza kati ya nchi hizo mbili licha ya kwamba nchi hizo zote ni wanachama wa SADC na nchi za SADC hazina viza kwa raia wake.
Je, ni kwa nini Serikali ya Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo haziondoi viza kwa raia wake ili kudumisha biashara kati ya wananchi wake kwa lengo la kukuza Kigoma kuwa Kituo cha Biashara cha Maziwa Makuu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge napenda kumfahamisha kuwa suala la kutotozana viza ni la kimakubaliano baina ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na si kwamba nchi za SADC hazina viza kwa raia wanaotaka katika nchi moja kwenda nchi nyingine.
Mheshimiwa Spika, katika nchi za SADC ilikubaliwa kuwa kila nchi wanachama ziwekeane utaratibu na namna bora ya kuondoa hitaji la viza kwa raia wao. Kwa sasa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wenye pasipoti za kidiplomasia na utumishi hawahitaji kulipia viza kuingia Tanzania.
Mheshimiwa Spika, Tanzania na DRC zimekuwa katika mazungumzo ya muda mrefu kuhusu namna bora ya kuondoa malipo ya viza kwa raia wake wenye pasipoti za kawaida, lakini mazungumzo hayo yamechelewa kukamilika kutoka na migogoro ya ndani iliyoko katika nchi ya DRC. Hata hivyo, ni mategemeo kuwa kupatikana kwa suluhisho la kudumu la migogoro iliyoko ndani ya nchi ya DRC kutawezesha kukamilishwa kwa taratibu za kuondoa hitaji la viza baina ya hizo nchi hizi mbili kwa haraka.