Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 6 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 75 2017-09-12

Name

Ahmed Juma Ngwali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ziwani

Primary Question

MHE. AHMED JUMA NGWALI aliuliza:-
Tanzania ilibadilisha Sera yake ya Kibalozi ili kuendana na mazingira ya sasa ya kiuchumi duniani kwa maana ya kujiwekeza katika Diplomasia ya Uchumi (Economic Diplomacy).
(a) Je, ni lini Tanzania ilibadili Sera yake ya Mambo ya Nje ya awali na kujielekeza katika Sera ya Diplomasia ya Uchumi?
(b) Je, mwenendo ukoje kati ya sera hii na ile iliyokuwepo awali?
(c) Je, ni vigezo au vipimo gani vinavyotumika kupima Balozi zetu katika utekelezaji wa sera hii ya Diplomasia ya Uchumi.

Name

Dr. Susan Alphonce Kolimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ahmed Juma Ngwali, Mbunge wa Wawi, lenye vipengele (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, mara baada ya Tanzania kupata uhuru mwaka 1961 na hata baada ya Muungano mwaka 1964, Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania iliweka msisitizo zaidi kwenye masuala ya kisiasa hususan kupigania uhuru wa nchi za Afrika zilizokuwa zinatawaliwa na wakoloni, kupanga ubaguzi wa rangi na ukoloni mamboleo.
Mheshimiwa Spika, ushiriki wa Tanzania kwenye masuala ya uhusiano wa Kimataifa kabla ya mwaka 2001 uliongozwa na matamko mbalimbali ya Viongozi Wakuu wa nchi na nyaraka kama vile Waraka wa Rais Namba 2 wa mwaka 1964. Tanzania ilifanikisha jukumu hilo kwa ufanisi mkubwa na kujijengea heshima mbele ya jamii ya Kimataifa.
Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilisha jukumu la kuzikomboa nchi za Afrika kutoka katika makucha ya ukoloni na vilevile kutokana na mabadiliko yaliyotokea duniani katika medani za kisiasa na uchumi ikiwemo kwisha kwa vita baridi, kuibuka kwa utandawazi, dhana ya demokrasia na uchumi wa soko, Tanzania ililazimika kubadili mwelekeo wa sera yake ya mambo ya nje.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo, mwaka 2001 Serikali ilitunga sera mpya ya mambo ya nje ambayo imeweka msisitizo kwenye diplomasia ya uchumi. Sera hiyo ndiyo inayoendelea kutekelezwa hadi hivi sasa.
(b) Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika jibu langu kwenye kipengele (a), sera ya awali ya mambo ya nje ilijikita zaidi katika masuala ya kisiasa ambapo Tanzania ilishiriki kikamilifu kutafuta ukombozi wa nchi nyingi za Bara la Afrika.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Sera ya Mwaka 2001 ya Mambo ya Nje ambayo utekelezaji wake umelenga zaidi kupata manufaa ya kiuchumi kutokana na mahusiano yake na nchi nyingine duniani, Tanzania imeshuhudia ongezeko kubwa la watalii waliotembelea nchi yetu; ongezeko kwenye biashara ya nje na uwekezaji, pamoja na kupatikana kwa mikopo yenye masharti nafuu na misaada ya kutekeleza miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika, licha ya kuwa sera ya sasa imejikita katika masuala ya kiuchumi, bado Tanzania inashirikiana na Jumuiya za Kikanda na Kimataifa katika kulinda amani na usalama katika nchi mbalimbali duniani.
(c) Mheshimiwa Spika, vigezo vinavyotumika kupima utendaji wa Balozi zetu ni pamoja na namna Balozi anavyotimiza majukumu yake kama yanavyoainishwa katika OPRAS na Mpango Kazi wake wa mwaka pamoja na kutekeleza kwa weledi majukumu yake kama kuvutia wawekezaji kutoka nje, kutafuta masoko ya bidhaa zetu, kuvutia watalii, kutafuta teknolojia sahihi na rahisi, kutafuta misaada ya maendeleo na mikopo ya masharti nafuu na kuendelea kujenga sifa nzuri ya nchi yetu na mambo hayo yamewekwa katika kitabu chao cha Ambassador’s Handbook.