Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 28 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 231 2017-05-18

Name

Ally Abdulla Ally Saleh

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Malindi

Primary Question

MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-
Tanzania imesajili michezo kadhaa ambayo huingia kwenye medani ya Taifa kiushindani lakini kote huwa ni mashamba yanayozaa visingizio.
(a) Je, Serikali haioni haja sasa ya kujipinda katika michezo michache kiushindani Kimataifa?
(b) Je, kama kukiwa na uamuzi huo inaweza kuwa michezo ipi?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imesajili michezo mbalimbali kwa kuzingatia sera, sheria, kanuni na taratibu zilizopo. Aidha, ili timu au mchezaji aweze kushiriki katika mashindano ya kimataifa kama vile michezo ya Olympic na michezo mingine, lazima awe amefikia viwango vilivyowekwa na mashirikisho ya kimataifa. Serikali inatoa mwanya kuibua na kukuzwa kwa vipaji katika michezo mbalimbali bila upendeleo. Suala la kufanya vizuri katika mashindano linategemeana na viwango vya uelewa, mazoezi, mafunzo na uzoefu katika mchezo husika.
Aidha, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inatoa msaada wa hali na mali kufanikisha timu ama mchezaji aliyefikia viwango kushiriki michezo ya Kimataifa ikiwa taarifa na taratibu zinazingatiwa tangu ngazi za awali. Kitendo cha kuchagua michezo kadhaa kinaweza kupelekea kupoteza vipaji ambavyo havijavumbuliwa na kukuzwa kufikia kushiriki mashindano kitaifa na kimataifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo Serikali itaendelea kuhamasisha michezo yote kupitia vyama vya michezo kwa sababu kila mchezo unaweza kushiriki kiushindani. Hii inasaidia kutoa fursa kwa wanamichezo wenye vipaji tofauti kuweza kushiriki katika michezo ya kimataifa.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, maoni ya Mheshimiwa Mbunge ni mazuri kwa maana ya kujikita katika michezo ile ambayo tunadhani itaweza kusaidia Taifa kufanya vizuri katika ushindani kimataifa, hili litawezekana kwa kusaidia timu ama mchezaji aliyefuzu, kwani katika hali halisi huwezi kuamua kuwa huu ndio mchezo unaoweza kufanya vizuri bila kupata viwango.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, niseme kuwa kwa sasa bado utaratibu huu hatujaanza kuutumia na kwa hiyo sio rahisi kujua ni michezo gani kwani kila mchezo unaandaliwa kwa kufuata taratibu na viwango husika na matokeo mazuri yanapatikana kwa kuibua na kukuza vipaji. Kwa kuchagua michezo kadhaa tutakatisha tamaa ukuaji wa vipaji katika michezo mingine. Lakini bado iko fursa kama wadau kufanya upembuzi wa kina na kuja na maoni juu ya michezo gani tuipatie kipaumbele kwa manufaa ya Taifa.(Makofi)