Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 21 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 183 2017-05-10

Name

Taska Restituta Mbogo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-
Mkoa wa Katavi ni miongoni mwa mikoa ambayo ina vivutio vingi vya utalii kama vile Mbuga ya Katavi yenye wanyama wengi, kivutio cha pekee cha twiga weupe ambao hawapatikani mahali pengine popote duniani:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kukitangaza kivutio hiki pekee cha utalii?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Katavi ni miongoni mwa mikoa yenye vivutio vingi vya utalii, vikiwemo Mbuga ya Wanyama ya Katavi, Mti wa Mzimu wa Katavi pamoja na vivutio vingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Bodi ya Utalii Tanzania na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania, imekuwa ikitangaza vivutio vya utalii vya Katavi kwa ujumla wake kupitia mitandao na tovuti mbalimbali za kijamii. Aidha, Majarida ya Utalii ya TANAPA na TTB yanayotolewa kwa lugha za Kiswahili, Kingereza, Kidachi, Kichina, Kifaransa na Kirusi ni sehemu ya njia zitumikazo katika kutangaza utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya Majarida hayo ni Selling Tanzania na Explore Tanzania yatolewayo na TTB na TANAPA Today na Hifadhi za Taifa Tanzania au Tanzania National Parks yanayotolewa na TANAPA. Aidha, TANAPA hutangaza pia utalii kupitia kipindi maalum kiitwacho Hifadhi za Jamii za Taifa kilichorushwa na Kituo cha Luninga cha Taifa (TBC). Kipindi hiki hurushwa kila wiki na kupitia kipindi hiki vivutio vinavyopatikana Hifadhi ya Taifa ya Katavi, kikiwemo kivutio pekee cha twiga weupe hutangazwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa ukarabati mkubwa wa Uwanja wa Ndege wa Mpanda kulikofuatiwa na ujio wa Ndege za Shirika la Ndege la Taifa (ATCL) kutasaidia sana kuongezeka kwa idadi ya watalii ambao watatembelea maeneo mbalimbali Mkoani Rukwa, ikiwemo Hifadhi ya Katavi. TTB na ATCL wanakamilisha matayarisho ya kuanzisha safari maalum za siku za mwisho za juma na siku za sikukuu kwa lengo la kuhamasisha na kuwawezesha Watanzania wengi zaidi kutembelea vivutio vya utalii vilivyoko Katavi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Bodi ya Utalii, Shirika la Hifadhi za Taifa la TANAPA na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro itaendelea kuboresha mbinu zilizopo na kubuni mbinu mpya, ili kuimarisha utangazaji wa vivutio vya utalii na hatimaye kuvutia watalii wengi zaidi katika sekta ya utalii nchini.