Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 27 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 222 2017-05-17

Name

Zubeda Hassan Sakuru

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-
Magereza mengi nchini hayapo katika viwango na ubora unaotakiwa na hivyo kuvunja haki za wafungwa.
Je, Serikali ina mkakati gani katika kufanya matengenezo na kulinda haki za wafungwa?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Magereza limekuwa likitekeleza na kusimamia haki za wafungwa magerezani kwa kuzingatia Sheria ya Magereza Na. 34 ya mwaka 1967 (The Prisons Act. No. 34 of 1967 CAP. 58 R.E 2002) pamoja na sheria nyingine na Kanuni za Uendeshaji wa Magereza za mwaka 1968 (The Prisons (Prison Management) Regulations of 1968) G.N.19 of 23/01/1968 na marekebisho yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, haki za wafungwa zinazotekelezwa na kusimamiwa magerezani kwa mujibu wa Sheria ya Magereza na Kanuni zake nilizozitaja au msingi mwingine, chimbuko lake ni Mkataba wa Kimataifa unaohusu Taratibu na Haki za Wafungwa na Mahabusu. Haki hizo zimeainishwa wazi sehemu ya VII na IX ya Sheria ya Magereza na Kanuni za Uendeshaji wa Magereza kama ifuatavyo:-
(i) Haki ya kutenganishwa ambapo wafungwa hutenganishwa kutokana na umri wao, jinsia, aina ya kosa, afya na tabia.
(ii) Haki ya kupatiwa chakula na mahitaji mengine. Mfungwa hupewa chakula kama ilivyoainishwa na Kanuni za Uendeshaji wa Magereza niliyoitaja.
(iii) Haki ya kuwa na uhuru wa kupata mawasiliano na kutembelewa na ndugu na jamaa zake. Mawasiliano haya ni pamoja na kupokea na kuandika barua, kusoma magazeti na kusikiliza taarifa mbalimbali kutoka katika vyombo vya habari.
(iv) Huduma za afya. Huduma hizi hutolewa kwa mfungwa pindi anapoumwa wakati wote awapo gerezani.
(v) Haki ya kupatiwa malazi safi na ya kutosha ambapo mfungwa mmoja anahitaji eneo la mita za mraba 2.8.
(vi) Haki ya kukata rufaa pale anapoona hakutendewa haki katika hukumu iliyotolewa na Mahakama dhidi yake.
(vii) Haki ya kucheza michezo. Mfungwa anayo haki ya kushiriki na kucheza michezo ya aina mbalimbali na hii inafanyika magerezani.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, zipo changamoto kwa Jeshi la Magereza zinazojitokeza katika kutekeleza baadhi ya haki hizo kutokana na msongamano wa wafungwa katika baadhi ya magereza na kutokana na hali halisi katika baadhi ya maeneo hayo niliyoyataja.(Makofi)